Wanawake waliovunja rekodi katika kujifungua pacha wengi

Mji wa  Igbo-Ora nchini Nigeria ni kati ya miji inayorekodi idadi kubwa ya visa vya kuzaliwa kwa watoto pacha duniani.

0

Mwanamke mmoja amejifungua watoto saba mjini Abbottaba nchini Pakistan. Rukhsana na mumewe wamejaaliwa wavulana wanne na wasichana watatu.Kulingana na maafisa wa afya hospitalini ni kuwa watoto walizaliwa wakiwa wamefikisha wiki 32 badala ya wiki 36 inavyostahili.

Rukhsana mwenye umri wa miaka 34 na mumewe Yar Mohammad walikuwa na watoto wengine wawili kabla ya kujaliwa pacha hao saba.

Mapema mwaka huu mwanamke kutoka Mali alijifungua watoto tisa, wawili zaidi kuliko madaktari walivyodhania baada ya kufanyiwa uchunguzi.

Halima Cissé mwenye umri wa miaka 25 alijifungua pacha hao nchini Morocco baada ya serikali ya Mali kumsafirisha hadi nchini humo.

“Nimejawa na furaha baada ya kuzaliwa kwa watoto wangu, mke wangu na watoto wako salama.” Alisema mumewe Halima.

Halima Cisse, aliyejifungua pacha tisa

Mwanamke aliyejifungua watoto nane nchini Marekani mwaka wa 2009 alikuwa anashikilia rekodi ya Guiness World Records.

Katika miaka ya nyuma, mwaka wa 1971 mwanamke kutoka Australia alijifungua watoto tisa na baadae mwaka wa 1999 mwanamke mwingine kutoka Malaysia pia alijifungua watoto tisa, ila katika visa vyote viwili watoto hao waliaga dunia baada ya siku kadhaa.

Kabla ya pacha wa Halima Cissé kuzaliwa mwezi Mei mwaka huu, mwanamke mwingine kutoka Amerika Nadya Suleman alikuwa anashikilia rekodi ya dunia kwa kujifungua watoto nane.

Nadya Suleman,aliyejifungua pacha nane

Mwezi Juni mwaka huu, mwanamke mwingine nchini Afrika Kusini anasemekana kujifungua pacha 10.

Gosiame Thamara Sithole mwenye umri wa miaka 37, alijifungua wavulana saba na wasichana watatu katika hospitali ya Pretoria.

Kulingana na uchunguzi wa madaktari, Gosiame alikuwa mjamzito na watoto nane kwa hiyo walishangazwa sana alipojifungua pacha kumi.

Sithole alijifungua watoto watano kwa njia ya kawaida na watano kwa upasuaji na alikuwa tayari na pacha wawili aliojifungua awali wenye umri wa miaka 6 sasa.

Gosiame Thamara Sithole , anasemekana kujifungua pacha kumi.

Guinness World Records inachunguza kisa hicho kubaini kama kweli Sithole alijifungua pacha 10.

Mji wa  Igbo-Ora nchini Nigeria ni kati ya miji inayorekodi idadi kubwa ya visa vya kuzaliwa kwa watoto pacha duniani.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted