22 wakamatwa kwa tuhuma za mauaji

Jeshi la Polisi jijini Mbeya nchini Tanzania linawashikilia watu 22 kwa tuhuma za kuhusika na matukio ya mauaji ambayo yametokea jijini humo.

0
Kamanda wa Polisi mkoani Mbeya, Urlich Matei

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne Februari 8, 2022, Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Mbeya, Urlich Matei amesema katika operesheni na msako mkali uliofanywa maeneo mbalimbali jijini humo, limewakamata watuhumiwa hao kwa makosa ya kuhusika na matukio hayo.

Hivi karibuni kumekuwapo na matukio kadhaa ya mauaji, yakiwamo ya aliyekuwa mwalimu mstaafu, Edwaerd Ndonde aliyeuawa na mwanaye Mussa Edward Januari 12, aliyekuwa Mwenyekiti wa Mtaa wa Hasanga ambayeni ni  Justine Namwinga naye aliuawa na watu wasiojulikana Januari 31 huku Gloria Kibira aliyekuwa Afisa Ustawi mwandamizi aliyekutwa amenyongwa nyumbani kwake Februari 3 mwaka huu.

Kamanda Urich amesema katika upelelezi uliofanywa na Jeshi hilo, umebaini vyanzo vya mauaji hayo ni ulevi, wivu wa kimapenzi, imani za kishirikina , migogoro ya ardhi, kuwania mali na kujichukulia sheria mkononi.

Aidha Kamanda Urich amesema “Watuhumiwa 16 kati ya 22 wamefikishwa mahakamani na wengine watafikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi wa mashauri yao kukamilika” amesema Matei.

 Urich amesema ili kukomesha matukio hayo, wananchi wanapaswa kuacha kujichukulia sheria mkononi kwa kuwafikisha watuhumiwa Polisi, viongozi wa serikali za Mitaa, Watendaji wa Kata kutumia mabaraza ya usuluishi kutatua migogoro ya ardhi na kuwatumia wataalamu waliopo katika kamati za ulinzi na usalama kutoa elimu ya namna ya kudhibiti msongo wa mawazo.

Matukio ya mauaji nchini humo yametikisa tangu kuingia mwaka 2022, ambapo hadi sasa zaidi ya matukio 20 yametokea katika kipindi cha Januari hadi sasa. 

Matukio hayo yamewaibua viongozi wakubwa wa nchi hiyo akiwemo Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan aliyetaka uchunguzi zaidi kufanyika juu ya matukio hayo lakini pia akiweka kitanzi kwa jeshi la polisi akiwaambia kuwa wanapaswa kujitathimini.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted