Makundi yenye silaha nchini DR Congo yanawashikilia wajumbe waliotumwa na rais

Walienda huko kwa dhamira kutoka kwa Rais Felix Tshisekedi ili kujadili masharti ya kusitisha mapigano na kuwakomesha uharifu katika eneo hilo.

0

Wababe watatu wa zamani wa kivita wanashikiliwa na wanamgambo kaskazini mashariki mwa DR Congo, ambapo walikuwa wamekwenda kwa nia ya kujadili kujisalimisha, duru zilisema.

Thomas Lubanga, Germain Katanga na Floribert Ndjabu na wajumbe wengine watano walizuiliwa siku ya Jumatano katika jimbo la Ituri.

Walienda huko kwa dhamira kutoka kwa Rais Felix Tshisekedi ili kujadili masharti ya kusitisha mapigano na kuwakomesha uharifu katika eneo hilo.

Ndjabu, aliyefikiwa kwa simu na AFP, alisema Jumatano alasiri kwamba wajumbe walikuwa katika kijiji cha Petsi “kwa mazungumzo na wanamgambo wa CODECO.”

“Tunashikiliwa na kundi hili kwa nia ya kuendelea na mazungumzo katika muktadha wa dhamira yetu,” alisema.

Jitihada zaidi za kufikia simu za wajumbe hao – unaojumuisha wababe watatu wa zamani wa vita, kanali wawili wa jeshi la Kongo na wasindikizaji watatu – zilishindikana.

“Kulikuwa na ufyatuaji wa makombora kutoka kwa jeshi wakati wa mkutano… kwa hivyo tuliamua kuwashikilia,” Basa Zukpa Gerson, msemaji wa kikundi cha CODECO, Muungano wa Wanamapinduzi wa Ulinzi wa Watu wa Kongo (URDPC), aliiambia AFP.

“Iwapo Rais Tshisekedi anataka kufanya mazungumzo, acha awaombe wanajeshi wake waondoke katika eneo hilo na tutazungumza.”

Lubanga na Katanga mtawalia walitumikia vifungo vya miaka 14 na 12 jela vilivyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) kwa uhalifu uliofanywa huko Ituri.

Ndjabu alifungwa jela miaka 15 kwa mauaji ya walinda amani tisa wa Umoja wa Mataifa.

CODECO — Ushirika wa Maendeleo ya Kongo — ni dhehebu la kisiasa na kidini ambalo linadai kuwakilisha maslahi ya kabila la Lendu.

Kulingana na mamlaka ya Umoja wa Mataifa na Kongo, kundi hilo ndilo linalochochea ghasia nyingi za sasa huko Ituri.

Linadaiwa kuwaua raia 18 siku ya Jumanne.

Ituri na jimbo jirani la Kivu Kaskazini yamewekwa chini ya hali ya kuzingirwa tangu Mei mwaka jana, lakini ukandamizaji huo hadi sasa umeshindwa kukomesha unyanyasaji unaofanywa na makundi yenye silaha.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted