Mbowe na wenzake walivyotoka kwenye kitanzi cha kesi ya Ugaidi

Ilikuwa inasubiriwa siku saa na dakika kuweza tu kujua hatma ya Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe na wenzake watatu, juu ya kupatikana kwa uhuru wao uliochukuliwa na dola.

0
Mohammed Abdillah Ligw’enya , Freeman Aikaeli Mbowe , Adam Hassan Kasekwa na Khalfan Hassan Bwire, wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kuachiwa huru.

Ilikuwa inasubiriwa siku saa na dakika kuweza tu kujua hatma ya Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe na wenzake watatu, juu ya kupatikana kwa uhuru wao uliochukuliwa na dola.

Hii leo Machi 4,2022  ndio siku na muda uliwadia baada ya Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, jijini Dar es Salaam, nchini Tanzania, kufuta kesi ya Uhujumu Uchumi yenye makosa ya Ugaidi ndani yake iliyokuwa inamkabili kiongozi huyo na wenzake kufuatia Wakili wa Serikali Mwandamizi, Robert Kidando, kuwasilisha hati ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), Sylvester Mwakitalu ya kutokuwa na nia ya kuendelea na kesi hiyo.

Lakini je kabla ya uamuzi huo nini kilitokea.

Itakumbukwa kuwa leo ndio siku ambayo Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi. ilipanga kuanza kusikiliza utetezi baada ya mahakama hiyo kuwakuta na kesi ya kujibu Mbowe na wenzake, umaumuzi ambao ulitolewa Februari 18,2022.

Kesi hii ilipaswa kuanza mishale ya saa 3 asubuhi lakini hadi majira ya saa 4:52, Magereza hawakuwafikisha Mbowe na wenzake katika viunga vya mahakama hiyo.

Pamoja na hayo usikilizwaji wa kesi hiyo ulichelewa, lakini hadi kesi inakuja kuanza tayari mshale wa saa ulikua unasoma majira ya saa tano asubuhi.

Wanachama wa CHADEMA kwa umoja wao walikusanyika mahakamani hapo kama kawaida yao, wakitokea sehemu mbalimbali ikiwemo nje ya mkoa wa Dar es salaam, lakini wengi wao wakiamini kuwa Mbowe atarudi uraiani.

Majira ya saa tano Jaji Tiganga ambaye alikua anasikiliza kesi hiyo ameingia na usikilizwaji wa kesi ukaanza ambapo, Wakili utetezi Peter Kibatala kwa niaba ya mawakili wenzake aliiambia mahakama kua shauri hilo leo lilikwenda mahakamani hapo kwa ajili ya ya utetezi na kwamba tayari walishaonana na wateja wao siku ya Jumamosi na Jumapili ambazo walikwenda kuwatembelea kwenye gereza la ukonga na Segerea, huku wakiamini kuwa leo mahakama ingeanza kusikiliza utetezi wa watuhumiwa.

Hata hivyo Kibatala amesema kuwa mapema leo asubuhi alipata taarifa kutoka kwa askari magereza kwamba Mbowe amepata matatizo ya kiafya hivyo ameshindwa kuhudhuria mahakamani.

“Mheshimiwa Jaji ni kweli kwamba shauri lilikuwa limepangwa kwa ajili ya utetezi. Kwa upande wangu tulifanya maandalizi mazuri sana. Mimi, John Mallya, Dickson Matata, Fredrick Kihwelo na wengine juzi na jana tulikuwa Ukonga na Segerea. Tulikutana nao wakiwa na bashasha kabisa, kwamba leo tunaendelea na utetezi. Lakini leo ssubuhi tumepata taarifa kutoka kwa askari Magereza kwamba Mbowe amepata matatizo ya kiafya. Kwa hiyo hatuwezi kuendelea. Tunaweza kupanga kuendelea Jumatatu.” amesema wakili Peter Kibatala

Hoja hiyo ya Kibatala haikuweza kupingwa na upande wa Jamhuri isipokuwa Wakili wa Serikali Robert Kidando alikiri kwa kumwambia Jaji, kwamba shauri hilo limekuja kwa ajili ya utetezi, na wamesikia maombi ya utetezi kuhusu washtakiwa lakini Mkurugenzi Wa Mashitaka (DPP) kwa niaba ya Jamhuri ameomba kuwasilisha taarifa ya kutokuwa na nia na kuendelea na shauri hilo

“Mheshimiwa Jaji tunaomba moja la kufanya mbele ya Mahakama yako. Na ombi hili Mheshimiwa Jaji ni kwamba Mkurugenzi Wa Mashitaka (DPP) kwa niaba ya Jamhuri anaomba kuwasilisha taarifa ya kutokuwa na nia na kuendelea na shauri hili” amesema Robert Kidando, Wakili wa Serikali

Taarifa hiyo imetolewa  chini ya Kifungu cha 91(1) kwa Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai na imewasilishwa kwa njia ya maandishi, kwa maombi hayo hayo ya kifungu cha 91(1), hivyo mashtaka yote yaliyokuwa yanawakabili washtakiwa yameondolewa.

Baada ya Mahakama kusikiliza hoja iliyoletwa na wakili mwandamizi wa Serikali kwamba Mkurugenzi wa Mashitaka hana nia ya kuendelea na kesi hiyo,  na upande wa utetezi wakaridhia, Jaji aliyekuwa akiisikiliza kesi hiyo Jaji Jochim Tiganga amesema shauri hilo lililokuwa linawakabili washitakiwa Khalfani Bwire, Adam Kasekwa, Mohammed Ling’wenya na Freeman Mbowe limeondoshwa mahakamani na washitakiwa wanaachiwa huru bila masharti. 

Aidha Jaji Tiganga amesema anaandaa amri ya kuviachia vielelezo vyote vilivyoletwa Mahakamani wakati wa kesi hiyo ilipokuwa ikisikilizwa na huku akimuelekeza Mkuu wa Magereza kuwaachia huru Mbowe na wenzake  hii leo.

“Kwa sababu kuna vielelezo vililetwa Mahakamani, naandaa Amri ya kuviachia, na hivyo naelekeza Mkuu wa Magereza kuwaachiwa mara moja leo na si vinginevyo. Natoa amri”mawakili wa utetezi katika kesi hiyo walitoa jasho na damu lao mahakamani hapo, kuhakikisha Mbowe na wenzake wanaachwa huru.

Uamuazi huo wa Mahakama uliibua ndelemo ndani ya Mahakama na nje ya mahakama.

Hali ilikuaje nje ya Mahakama?

Nje ya Mahakama waweza sema kuna sherehe, kila mmoja akicheza kwa style yake anayoijua.

Ni nyimbo za ushindi ndizo zilitawala na cha kushangaza zaidi vyombo vya dola vilivyokuwa katika viunga vya ahakama hiyo viliwaacha tu wanacahama hao waendelee kufurahia uamuazi huo.

Wakili Kibatala amewaambia wanahabari kuwa mawakili wa utetezi katika kesi hiyo walitoa jasho na damu lao mahakamani hapo, kuhakikisha Mbowe na wenzake wanaachwa huru.

“Mimi binafsi nianze kwa kushukuru jopo la mawakili ambao pamoja nami walipigana kiume na kike kwa kutegemea jinsia zao,” amesema Kibatala na kuongeza kuwa .

“Tanzania na dunia nzima imeshuhudia hakuna kitu chochote tumekiacha, tumetoa jasho, damu na mioyo yetu tumeiacha mahakamani. Ninasikia fahari mawakili wenzangu ambao walikuwa hawafahamiki wao nani wanafahamika na kazi zao zinajukikana,” amesema Wakili Kibatala.

Pamoja na kufuruahia uamuzi ulitolewa na DPP, kibatala amesema safari katika kesi hiyo ilikuwa ni ndefu katika kesi hiyo licha ya uzoefu aliokuwa nao lakini ameweza kupambana kadiri ya uwezo wake na mawakili wenzake

“Safari ilikuwa ndefu, nilisimamia kesi tatu za ugaidi watu wakaachiwa huru, lakini hii impact yake ilikuwa kubwa. Cha msingi tulijitahidi kutumia ujuzi wetu wote hata pale palipokuwa na mabonde tulijua safari yetu itaishia wapi,” amesema Wakili Kibatala na kuongeza:

“Ni safari ndefu sio kazi rahisi, nimesimamia hii kesi ya Mbowe ambayo inatazamwa nchini na duniani kote. Presha zilikuwa kubwa tuko very proud tuliacha kila kitu chetu mahakamani, dunia na nchi mliiona hilo,” amesema

Wakili Peter Kibatala ndiye aliyekuwa akimuwakilisha Freeman Mbowe katika kesi hiyo, ambapo amebainisha kuwa ameweza kusimamia kesi tatu za ugaidi na kuweza kushinda kesi zote.

Kesi ya Mbowe ilivyotazamwa kwa jicho la pekee

Tangu kuanza kwa kesi hii imekuwa ikifuatiliwa kwa ukaribu zaidi kutoka ndani na nje ya Tanzania.

Vyombo vya habari vya ndani ya Tanzania vimeripoti kesi hii tangu siku ya kwanza hadi hii leo ilipofikia maamuzi ya kuondolewa, hivyohiyvo kwa vyombo vya habari vya nje Tanzania.

Hata hivyo Balozi, Mashirika ya Kimataifa ya Haki na mashirika ya haki kwa Tanzania, Wanaharakati, viongozi wa dini na wanasiasa wamekuwa wakiifatilia kesi hii katika kila hatua, na hata baadhi ya mabalozi waliweza kuhudhuria mahakamani wakati wa uskilizwaji wa kesi hiyo.

Mtazamo wa watu kwenye kesi hii

Baadhi ya wakosoaji aliitazama kesi hii ni kama kesi ya ukandamizaji kisiasa na imetumika kama sehemu ya kuukandamiza upinzani nchini Tanzania.

Itakumbukwa kuwa kwa zaidi ya miaka mitano sasa wanasiasa wa siasa za upinzani nchini Tanzania wamekuwa wakilalamika juu ya ukandamizwaji wa uhuru wa siasa nchini humo huku wakiilaumu zaidi serikali iliyopo mamlakani.

Wanachama wenyewe wa CHADEMA waliita kesi hii ni kesi ya “MCHONGO” yaani ni kama kesi ya kubambikiwa ili hali hakuna kesi.

Yaliyojiri kwenye kesi ya Mbowe tangu imeanza

Itakumbukwa kesi hii ilianza rasmi kusikilizwa mnamo mwezi Septemba katika Mahakama Kuu Divisheni ya Rushwa na Uhujumu na Uhujumu Uchumi, ambapo Mbowe na wenzake walisomewa mashtaka sita likiwemo shtaka la ugaidi.

Katika kesi hiyo mawakili wa Jamhuri waliiambia Mahakama kuwa wangekuwa na mashahidi 24 lakini walileta mashahidi 13 na kufunga ushahidi wao.

Aidha kuliibuka mapingamizi takribani 9 yaliyoibuliwa na jopo la mawakili wa utetezi, ambapo katika mapingamizi hayo mawakili Wa utetezi walishinda pingamizi moja.

Kesi hiyo iliendeshwa na majaji watatu katika kipindi tofauti ambapo wawili walijiondoa kendelea kusikiliza kesi hiyo.

Jaji wa kwanza kujiondoa alikua ni Jaji Elinaza Luvanda, ambaye alijitoa baada ya washtakiwa kukosa imani nae.

Jaji wa pili alikua no jaji Mustapha Siyani ambaye alijiondoa baada ya kuteuliwa kuwa Jaji Kiongozi hivyo alibainisha kuwa hatoweza kuendelea kusikiliza kesi hiyo kutokana na majukumu mengi aliyonayo.

Jaji wa tatu ni jaji Joachim Tiganga ambaye ndiye jaji aliyesikiliza shauri hili hadi mwisho.

Mbali na Mbowe walioachiwa huru hii leo wengine ni Khalfani Bwire, Adam Kasekwa, Mohammed Ling’wenya 

Bwire, Kasekwa na Ling’wenya walikuwa askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) katika kikosi cha makomando kilichopo Sangasanga, mkoani Morogoro ambao wanadaiwa kuachishwa kazi kwa nyakati tofauti kwa sababu za kinidhamu

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted