Safari ya CDF Jenerali Mabeyo, katika kulitumikia Jeshi la Tanzania

Alizaliwa Julai 1, 1956 wilayani Magu mkoani Mwanza na kupata elimu ya msingi katika shule ya Namibu mkoani Mara kuanzia 1965 hadi 1971.

0

Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama nchini Tanzania(CDF), Jenerali Venance Mabeyo leo amemuaga Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Hussein Mwinyi baada ya kumaliza muda wake utumishi ndani ya Jeshi hilo.

Katika maelezo yake akiwa Ikulu ya Zanzibar, Mkuu huyo wa Majeshi ya Ulinzi, alieleza haja ya kumuaga pamoja na kutoa shukrani kwa Rais Mwinyi akieleza kuwa ni kiongozi ambaye amefanya naye kazi kwa muda mrefu na kumsaidia katika kutekeleza vyema majukumu yake ndani ya Jeshi hilo.

“Nakutakia afya njema na maisha marefu pamoja na familia yako….nathamini sana ushirikiano ulionipa katika kipindi chako cha uongozi tangu ukiwa Waziri wa Ulinzi hadi leo hii, ahsate sana”, amesem Jenerali Mabeyo

Mabeyo anafikia kikomo cha utumishi mwisho wa mwezi huu akiwa amelitumikia Jeshi hilo kwa kipindi cha miaka sita katika nafasi hiyo tangu alipoteulia na aliyekuwa Rais wa awamu ya tano hayati John Magufuli mwaka 2017.

Naye Rais Mwinyi mbali na kumpongeza kwa kutekeleza vyema majukumu yake katika kipindi cha utumishi wake ndani ya jeshi hilo, alimtakia kila la heri katika maisha yake ya kustaafu.

Ameuleza ushirikiano alioupata kutoka kwa Jenerali Mabeyo wakati akiwa Waziri wa Ulinzi na hata akiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwamba anauthamini na ataendelea kuukumbuka.

Lakini je Jenerali Venance Mabeyo ni nani hasa?

Jenerali Venance Mabeyo ni Mkuu wa Majeshi wa nane kuliongoza Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania tangu alipoteuliwa Februari 6, 2017 na aliyekuwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa awamu ya tano, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli.

Alizaliwa Julai 1, 1956 wilayani Magu mkoani Mwanza na kupata elimu ya msingi katika shule ya Namibu mkoani Mara kuanzia 1965 hadi 1971.

Alianza elimu ya Sekondari katika Seminari ya Nyegezi kuanzia 1972 hadi 1975, kisha akaendelea na kidato cha tano na sita Mzumbe Sekondari kuanzia 1976 hadi 1977. 

Jenerali Venance Mabeyo alijiunga na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania Januari 1, 1979 na kuhudhuria kozi ya afisa mwanafunzi na kupata kamisheni mwaka 1980 kuwa Luteni Usu.

Safari ya Jenerali Venance Mabeyo JWTZ

Julai 1980: Luteni Usu

Agosti 1981: Luteni

Januari 1987: Kapteni

Oktoba 1991: Meja

Juni 1998: Luteni Kanali

Mei 2006: Kanali

Septemba 2010: Brigedia Jenerali

Septemba 2014: Meja Jenerali

Juni 2016: Luteni Jenerali

Februari 2017: Jenerali

Jenerali Venance Mabeyo alihudhuria kozi mbalimbali ndani na nje ya nchi, baadhi ya nchi hizo ni Kenya, India, Canada na Marekani

Jenerali Venance Mabeyo katika kulitumikia Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania alishika nyadhifa mbalimbali ikiwemo Mwambata Jeshi nchini Rwanda, Msaidizi wa Mkuu wa Majeshi , Mkuu wa Tawi la Usalama na Utambuzi na Mnadhimu Mkuu wa JWTZ.

Jenerali Venance Mabeyo ametunukiwa medali mbalimbali;

Miaka 20 ya JWTZ

Medali ya utumishi mrefu.

Medali ya miaka 40 ya JWTZ.

Medali ya utumishi uliotukuka.

Medali ya Comoro na Anjouan.

Medali ya miaka 50 ya uhuru

Medali ya miaka 50 ya Muungano

Miaka 50 ya JWTZ

Miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted