Mkenya azuiliwa DR Congo kwa shambulio la bomu kanisani na kusababisha vifo vya watu 10

Tukio hilo la Kasindi, karibu na mpaka wa Uganda lilisababisha vifo vya watu 10 na liliacha takriban watu wengine 39 kujeruhiwa

0

Mamlaka ya Kongo inamshikilia Mkenya anayeshukiwa kuwa mwanachama wa kundi la kigaidi lililopigwa marufuku la Uganda, Allied Democratic Forces (ADF), na ambaye inasemekana ndiye aliyepanga shambulizi dhidi ya kanisa moja huko Kivu Kaskazini na kusababisha vifo vya watu 10 siku ya Jumapili.

Mamlaka ya Kongo haikutaja jina lake alipokamatwa siku ya Jumapili, lakini Kitengo cha Polisi cha Kupambana na Ugaidi nchini Kenya (ATPU) Jumatatu kilimtambua kuwa ni Abdirizak Muktar Garad mwenye umri wa miaka 29, anayetoka Kaunti ya Wajir, kaskazini mwa Kenya.

Tukio hilo la Kasindi, Kivu Kaskazini, karibu na mpaka wa Uganda liliacha takriban watu wengine 39 kujeruhiwa, kwa mujibu wa takwimu za awali za Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (FARDC).

Msemaji wa ndani wa Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (FARDC) Anthony Mualushayi Jumapili alisema kwamba, baada ya uchunguzi wa awali katika eneo la mkasa, Mkenya mmoja alikamatwa kwa kuwa na uhusiano na upangaji wa shambulio ambalo sasa linahusishwa na ADF.

Shambulio lenyewe lilikuwa bado halijadaiwa na makundi yoyote ya kigaidi, lakini jeshi la Kongo lililihusisha na ADF, kundi la kigaidi la Uganda lenye makao yake Mashariki mwa DR Congo, ambalo siku za nyuma lilishambulia vijiji vya DRC na kufanya mashambulizi katika maeneo ya mijini nchini Uganda. .

Magaidi hao wa ADF, ambao wengi wao wanaaminika kuwa na asili ya Uganda, wanaendesha shughuli zao Kivu Kaskazini na Ituri, mashariki mwa DRC.

Mnamo Januari 2022, Mkenya mwingine, Salim Rashid Mohamed almaarufu Chotara, alikamatwa nchini DRC kufuatia miezi kadhaa ya kuwindwa na mamlaka ya Kongo. Vyombo vya usalama vya DRC vilidai kuwa mtandao wa magaidi umeanzishwa nchini DRC na kuwavutia watu fulani kutoka Afrika Mashariki. Salim na washukiwa wengine kadhaa walisemekana kuvuka hadi DRC kupitia Uganda.

Kulingana na FARDC, shambulio la kigaidi siku ya Jumapili “lilipiza kisasi kwa hasara ambayo magaidi hao wameipata katika medani kadhaa za vita dhidi ya FARDC.”

Mara tu baada ya shambulio la Jumapili, serikali ya Kongo na jeshi waliwataka raia “kuwa macho na kuepuka mikusanyiko”, huku Rais Félix Tshisekedi akiahidi kuwa “wahusika watachukuliwa hatua na kuadhibiwa vikali.”

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted