Prof Kithure Kindiki ni nani?

Rais William Ruto amemteua Waziri wa Usalama profesa kithure kindiki kuwa naibu rais  baada ya kuondolewa madarakani kwa Rigathi Gachagua. Tayari bunge la kitaifa limemuidhinisha na na sasa anasubiri kuapisha rasmi. Na je, Profesa Kindiki  ni nani?

Abraham Kithure Kindiki alizaliwa tarehe 17 Julai 1972) na ni mwanasiasa na wakili wa Kenya ambaye ni Waziri wa Mambo ya Ndani na Utawala wa Serikali ya Kitaifa. Aliwakilisha Kaunti ya Tharaka-Nithi katika Seneti ya Kenya kuanzia 2013 hadi 2022.

Alichaguliwa kwa mara ya kwanza mwaka wa 2013 na kuchaguliwa tena mwaka wa 2017.

Alikuwa Kiongozi wa Wengi katika Seneti katika kipindi cha 2013-2017 na Naibu Spika wa Seneti kuanzia Agosti 2017 hadi 2020.

Akiwa wakili wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC), Prof. Kindiki alipata shahada ya Sheria  kutoka Chuo Kikuu cha Moi na Diploma ya Mafunzo ya Sheria kutoka Shule ya Sheria ya Kenya.

Pia ana Shahada ya Uzamili katika Sheria ya Kimataifa ya Haki za Kibinadamu na Demokrasia na Shahada ya Uzamivu katika Sheria za Kimataifa, kutoka Chuo Kikuu cha Pretoria, Afrika Kusini.

Mapema katika taaluma yake, Prof. Kindiki alikuwa mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Moi.

Pia aliwahi kuwa Mhadhiri Mwandamizi na Mkuu wa Idara ya Sheria ya Umma katika Chuo Kikuu cha Nairobi.

Alipanda hadi kuwa Muhadhiri Mshiriki katika Shule ya Sheria katika taasisi hiyo hiyo.

Pia aliwahi kuwa Katibu wa Uwiano wa Kitaifa chini ya Rais Mwai Kibaki.

Msomi huyo mashuhuri katika sheria za Kimataifa na haki za binadamu, amewahi kuwa mshauri wa mashirika ya ndani na kimataifa ikiwa ni pamoja na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) na Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP) miongoni mwa mengine.

Yeye ni mwanachama wa Baraza kuhusu Mfumo wa Umoja wa Mataifa (ACUNS), Chama cha Kimataifa cha Utafiti wa Uhamiaji wa Kulazimishwa (IASFM), Chama cha Wanasheria wa Kenya (LSK) na Tume ya Kimataifa ya Wanasheria, Kenya (ICJ- K).