Mashirika ya haki za binadamu nchini Kenya yamepanga maandamano ya amani tarehe 24 Februari 2025 jijini Nairobi, wakitaka kuachiliwa kwa Dr. Kizza Besigye, kiongozi wa upinzani wa Uganda ambaye amezuiliwa kwa zaidi ya miezi mitatu.

Besigye alitekwa nyara jijini Nairobi tarehe 16 Novemba 2024, alipokuwa akijiandaa kuhudhuria uzinduzi wa kitabu cha Martha Karua, kisha alirejeshwa kwa nguvu nchini Uganda, ambako alifunguliwa mashtaka katika mahakama ya kijeshi. Kukamatwa kwake kumeibua ghadhabu, huku wanaharakati wakilaumu serikali ya Uganda kwa kuminya wapinzani wa kisiasa na kukiuka sheria za kimataifa za haki za binadamu.
Licha ya uamuzi wa Mahakama ya Juu ya Uganda tarehe 31 Januari 2025 kwamba raia hawapaswi kushtakiwa katika mahakama za kijeshi, Besigye na wafungwa wengine wa kisiasa bado wanashikiliwa bila hatima ya kesi zao.
Mashirika ya haki za binadamu nchini Kenya, yakiwemo Amnesty International, Law Society of Kenya (LSK), na Kenya Human Rights Commission (KHRC), yameapa kuchukua hatua. Wameandaa maandamano ya amani tarehe 24 Februari, ambayo yatafanyika kwa hatua mbili:
- Saa 4 asubuhi (10am): Waandamanaji watakusanyika katika Aga Khan Walk na kuandamana hadi Bunge la Kenya kuwasilisha madai yao.
- Saa 8 mchana (2pm): Maandamano yataendelea kutoka Riverside Square hadi Ubalozi wa Uganda huko Kileleshwa, ambako wanaharakati watatoa wito wa kuachiliwa kwa Besigye na haki kwa wafungwa wote wa kisiasa nchini Uganda.
Maria Sarungi kutoka Change Tanzania Movement alikosoa vikali hatua ya Uganda, akisema, “Utekaji nyara nchini Uganda ni sawa na utekaji nyara nchini Kenya na Tanzania. Hatutakubali ukiukaji wa haki za binadamu, na tunasisitiza kuheshimiwa kwa haki za raia wa Afrika Mashariki.”
Mashirika haya yanaitaka serikali ya Uganda iwaachilie mara moja Dr. Besigye, Hajj Obeid Lutale, na wakili Eron Kiiza, na vilevile yasitishwe matumizi ya mahakama za kijeshi dhidi ya raia. Pia wanaitaka serikali ya Kenya ichunguze na ikomeshe visa vya utekaji nyara na kuwarejesha kwa nguvu wapinzani wa kisiasa walioko nchini humo.