Senegal yawakamata watatu kwa vifo vya watoto wachanga kwenye moto hospitalini

Polisi wa Senegal wamewakamata watu wa kwanza kwa kuhusiana na moto katika hospitali ambapo watoto 11 walifariki, duru za vyama vya wafanyakazi zilisema Jumatatu.

Moto huo ulizuka katika wodi ya watoto wachanga katika mji wa magharibi wa Tivaouane Jumatano iliyopita.

Rais Macky Sall alimfuta kazi waziri wake wa afya, Abdoudaye Diouf Sarr, siku moja baada ya mkasa huo.

Watu watatu waliokamatwa kuhusiana na kisa hicho ni mkunga, muuguzi na mkuu wa idara ya rasilimali watu ya hospitali hiyo, afisa wa chama cha wafanyakazi wa afya aliambia AFP.

Walikuwa wakihojiwa kwa tuhuma za ‘kuhatarisha maisha ya wengine,’ afisa Ousmane Diouf alisema.

Wataalamu hao wawili wa matibabu walikamatwa siku ya Jumapili.

Chanzo cha moto katika hospitali ya Mame Abdou Aziz Sy Dabakh hakijafahamika ingawa hitilafu ya umeme imetajwa kuwa chanzo.

Walioshuhudia waliripoti kuwa moto huo ulisambaa kwa kasi katika kitengo cha watoto wachanga na kwamba wafanyakazi na wagonjwa hawakuweza kuwaokoa watoto hao.

Ndugu na jamaa waliofiwa wamelalamikia ukosefu wa usimamizi katika wodi hiyo.

Meya wa eneo hilo Demba Diop amekanusha madai kutoka kwa jamaa na mitandao ya kijamii kuwa watoto hao waliachwa peke yao, akisema mkunga na nesi walikuwepo wakati moto huo ulipozuka.

Meya alisema kiyoyozi hicho ndicho kilichochea moto huo.

Wauguzi hao wawili walizirai lakini wakafufuliwa, aliongeza.

“Hakukuwa na uzembe,” alisisitiza.

Mkasa huo ulikuwa wa hivi punde zaidi katika mfululizo wa matukio mabaya yaliyoangazia mapungufu katika mfumo wa afya wa Senegal.

Siku ya Ijumaa, Global Mercy, meli kubwa zaidi duniani iliyojengwa kwa madhumuni ya hospitali ya kiraia, ilitia nanga mjini Dakar kwa muda wa wiki nne kutoa mafunzo kwa wataalamu wa afya.

Meli hiyo ya urefu wa mita 174 (futi 570) na uzani wa tani 37,000 ilikabidhiwa kwa hisani ya Mercy Ships na waunda meli wake Julai iliyopita.

Wakati ikiwa nchini Senegal “itakuwa fursa nzuri kwa shughuli za msaada za Global Mercy kufanya kazi inayoonekana barani Afrika kwa mara ya kwanza, kwa kuzingatia kujenga na kuboresha uwezo wa matibabu,” Mercy Ships alisema.

Rais Sall aliikaribisha rasmi meli hiyo katika bandari ya Dakar siku ya Jumatatu katika hafla iliyohudhuriwa pia na Rais wa Guinea-Bissau Umaro Sissoco Embalo na Rais wa Comoro Azali Assoumani,

Mawaziri wa afya wa Gambia, Cameroon na Jamhuri ya Congo pia walihudhuria.