Afisa Wa Afya Akamatwa Kwa Tuhuma Za Kumbaka Mama Mjamzito Bomet

Afisa wa afya nchini Kenya amekamatwa kwa tuhuma za kumbaka mama mjamzito katika Kituo cha Afya cha Chemaner katika kaunti ya Bomet.

Afisa Wa Afya Akamatwa Kwa Tuhuma Za Kumbaka Mama Mjamzito Bomet

Mashuhuda na ripoti za polisi zinaeleza kuwa Eric Langat, maarufu Kirinyet, alipatikana katika hali ya kutatanisha na mgonjwa ndani ya chumba cha ushauri baada ya wenzake kukimbilia kufuatia kelele za msaada.

Kamanda wa Polisi wa Bomet Mashariki, Michael Singa, alisema mlalamikaji alipiga kelele kuita usaidizi mara tukio lilipoanza, jambo ambalo lilizua hofu mara moja na kuvutia wahudumu na wagonjwa waliokuwepo ambao walifika kwenye chumba hicho kutaka kufahamu kilichokuwa kikijiri humo ndani.

Tukio hilo liliripotiwa mara moja katika Kituo cha Polisi cha Chemaner, na kupelekea operesheni ya kumtafuta mtuhumiwa.

Polisi walimfuatilia hadi mafichoni na kufanikiwa kumtia mbaroni.

Muathiriwa alipelekwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Longisa kwa uchunguzi wa kitabibu na usaidizi wa kisaikolojia.

Kamanda Singa alithibitisha kuwa mtuhumiwa atabaki rumande kwa mahojiano na atafikishwa mahakamani mara uchunguzi utakapokamilika.

Vyombo vya usalama vimesisitiza kuwa shauri hili litashughulikiwa kwa mujibu wa sheria, huku wakazi wakionyesha wasiwasi kuhusu usalama wa wagonjwa na uwajibikaji wa wahudumu wa afya.