Bei Ya Mafuta Kenya Yaongezwa Kwa Kiwango Cha Juu

Wakenya watalazimika kugharimika zaidi baada ya kupanda kwa bei za mafuta katika tathmini mpya iliyotangazwa na Halmashauri ya Kudhibiti Bei za Nishati na Mafuta, EPRA Alhamisi usiku.

Bei hizo mpya za mafuta zitatekelezwa kuanzia Septemba 15, usiku wa manane hadi Oktoba 14, 2023.

Katika taarifa iliyotolewa na halmashauri hiyo ikiashiria ongezeko kubwa la bei za mafuta nchini, lita moja ya mafuta ya petroli jijini Nairobi sasa itauzwa kwa shilingi 211.64 baada ya kuongezwa kwa shilingi 16.96, lita moja ya dizeli itauzwa kwa shilingi 200.99 baada ya kuongezwa kwa shilingi 21.32 wakati mafuta taa yakiuzwa kwa shilingi 202.61 kwa lita baada ya kuongezwa kwa shilingi 33.13.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa EPRA Daniel Bargoria, ongezeko hilo linatokana na ongezeko la kufikisha mafuta yaliyoagizwa nchini ambapo gharama za kusafirisha mafuta ya petroli hadi Mombasa ziliongezeka kwa asilimia 4.80, mafuta ya dizeli kwa asilimia 12.52 na mafuta taa kwa asilimia 19.79.