China: Mwanamume ashikiliwa kama ‘mtumwa wa damu’ na kutolewa damu kwa miezi kadhaa

Mwanamume mchina aliyeshawishiwa na tangazo la kazi azuiliwa kama “mtumwa wa damu” kwa miezi kadhaa nchini Cambodia.

Inaaminika kuwa genge lililomzuia lilimtoa damu na kuiuza mtandaoni kwa wanunuzi wa kibinafsi.

Mwanamume huyo karibu atolewe damu yote kabla kuwatoroka watekaji wake katika jiji la Sihanoukville, Cambodia.

Mwanamume huyo, aliyetambuliwa tu kwa jina lake la ukoo Li, alitekwa nyara na genge na kutumika kama “mtumwa wa damu” kwa miezi kadhaa, iliripoti South China Morning Post.

Tangu Agosti 2021 lilipomzuia Li, genge hilo liliripotiwa kuchukua takriban mililita 800 za damu kutoka kwa mwanamume huyo mwenye umri wa miaka 31 kila mwezi, na kumwachia muda wa kutosha tu kuongeza damu mwilini.

Uchangiaji wa kawaida wa damu kwa kawaida huchukua takribani mililita 470 za damu, ambayo ni takriban 8% ya wastani wa ujazo wa damu ya mtu mzima.

Ingawa mwili wa mwanadamu unaweza kurejesha kiasi hicho cha damu ndani ya saa 24 hadi 48, kujaza seli nyekundu za damu huchukua karibu wiki 10 hadi 12.

Ndiyo maana Shirika la Msalaba Mwekundu la Amerika linapendekeza kwamba mtu angoje angalau wiki nane (siku 56) kabla ya kuchangia tena.

Li alitolewa damu nyingi sana hivi kwamba watekaji wake walianza kumtoa damu kichwani mwake kwani mishipa ya mikononi mwake haikuweza tena kutoa damu ya kutosha.

Alifanikiwa kutoroka kwa usaidizi wa mmoja wa washiriki wa genge hilo mapema mwezi huu, lakini tayari alikuwa katika hali mbaya na  viungo vyake vingi vilikuwa vimeathirika.

Li alipolazwa hospitalini mnamo Februari 12, mikono yake ilikuwa na michubuko mingi na ilikuwa imejaa alama za sindano.

Kushikiliwa kwa Li

Li, ambaye hapo awali alifanya kazi kama mlinzi huko Shenzhen na Beijing, aliambia vyombo vya habari kwamba alishawishiwa na genge tofauti kuelekea Guangxi Zhuang kusini mwa China kupitia tangazo la kazi kutoka kwa kampuni feki.

Kulingana na Li, genge hilo liliamua kuchukua damu kutoka kwake baada ya yeye kukataa kujiunga na operesheni yao ya ulaghai mtandaoni. Chini ya tishio la kuuzwa kwa wavunaji wa viungo, Li alilazimika kuwaacha wachukue damu yake.

Genge hilo pia lilitumia vifaa vya umeme kumdhuru yeye na mateka wengine hadi wakubali kutolewa damu. Li alifichua kuwa kulikuwa na takriban wanaume wengine saba katika chumba walikokuwa wamezuiliwa.

Kwa sababu Li ana aina ya damu ya O-, genge hilo lilichukua damu nyingi kutoka kwake kuliko wanaume wengine.

Alikumbuka jinsi mtu ambaye alimpa damu yake hapo awali alisema kwa mshangao kwamba aina yake ya damu ilikuwa “ya thamani sana.”

Genge hili kisha likamteka nyara Li na kumleta kwenye mpaka wa China na Vietnam.

Baada ya kumlazimisha kuvuka mpaka, genge hilo lilimpeleka katika Jiji la Ho Chi Minh na hatimaye hadi Sihanoukville.

Mara tu walipofika Cambodia, genge lingine linaloendesha kampuni ya ulaghai mtandaoni lilimnunua Li kwa $18,500.

Kulingana na maelezo ya Li, washiriki wote wa magenge hayo ni Wachina na waliwafanya mateka hao  kama “zana za kupata pesa.”

Kwa sasa Li anapokea matibabu hospitalini na inasemekana hali yake inaendelea vizuri.

Katika taarifa, ubalozi wa China nchini Cambodia ulisema kuwa umetoa wito kwa mamlaka ya Cambodia kuchunguza kesi hiyo.

Mwakilishi wa ubalozi huo alimtembelea Li katika hospitali hiyo wiki hii.