Mwandishi wa riwaya wa Uganda na mkosoaji wa serikali akamatwa

Kakwenza Rukirabashaija, Mwandishi wa Riwaya

Mwandishi mashuhuri wa Uganda na mkosoaji wa serikali amekamatwa mjini Kampala, wakili wake alisema Jumatano. Wanaharakati wa haki wametoa wito wa kuachiliwa kwake.

Wanaume wenye silaha wanaodai kutoka kwa Jeshi la Polisi la Uganda “walivamia nyumba ya Kakwenza Rukirabashaija siku ya Jumanne,” wakili wake Eron Kiiza alisema, alikuwa akiongea na mteja wake kwenye simu alipokamatwa.

“Nilisikia wakimtishia kumvunja miguu,” Kiiza aliambia AFP.

Rukirabashaija ni mkosoaji mkubwa wa serikali ya Rais Yoweri Museveni, alipata sifa kwa riwaya yake ya kejeli ya mwaka 2020, “The Greedy Barbarian” ambayo inaelezea ufisadi wa hali ya juu katika nchi ya kubuni.

Rukarabashaija hivi majuzi alizidisha ukosoaji wa mwana wa Museveni Muhoozi Kainerugaba — jenerali ambaye Waganda wengi wanaamini anajiweka katika nafasi ya kuchukua nafasi ya babake mwenye umri wa miaka 77.

Haijabainika ni nani aliyemkamata mwandishi huyo. Rukirabashaija ni mshindi wa tuzo ya uandishi na kabla kukamtwa kwake aliandika kwenye ukurasa wake wa Facebook: “Wanaume wenye bunduki wanavunja mlango wangu. Wanasema wao ni polisi lakini hawajavaa sare.”

Kulingana na Kiiza, mashuhuda walimwona Rukirabashaija akiwekwa ndani ya gari linalojulikana kama “drone” ambalo huhusishwa na utekaji nyara wa wapinzani wa serikali nchini Uganda.

Rukirabashaija alichaguliwa na Tuzo ya PEN Pinter kushinda tuzo ya mwaka huu ya Mwandishi wa Kimataifa Jasiri, ambayo hutolewa kila mwaka kwa mwandishi ambaye amekuwa akinyanyaswa kwa kuzungumza kuhusu mambo anayoamini.

Rukirabashaija amekuwa akikamatwa mara kwa mara baada ya gazeti la “The Greedy Barbarian” kuchapishwa na kusema kuwa aliteswa wakati alipokuwa akihojiwa kuhusu kazi yake na majasusi wa kijeshi.

Wakati huo, alishtakiwa kwa kukiuka masharti ya kudhibiti kuenea kwa UVIKO 19 na kuchochea vurugu na kukuza madhehebu ya kupinga serikali.

Mwandishi huyo alielezea kuhusu wakati wake kizuizini kama “unyama na udhalilishaji” katika kitabu chake cha hivi karibuni “Banana Republic: Where Writing is Treasonous.”

Mapema mwezi huu Marekani iliweka vikwazo kwa mkuu wa kitengo cha kijasusi cha kijeshi cha Uganda, Abel Kandiho, ikimtuhumu kwa “kuongoza kuwahoji watu waliozuiliwa” wanaolengwa kwa mitazamo yao ya kisiasa.