Rais Ruto akutana na Rais Samia nchini Tanzania huku kukiwa na madai kwamba alimpuuza jijini Nairobi

Rais William Ruto akutana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu rasilimali watu jijini Dar-es-Salaam 26/7/2023

Rais William Ruto ametua Tanzania kukutana na mwenzake Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan.

Jumanne usiku kupitia akaunti yake ya Twitter, Rais William Ruto alitangaza kuwa yuko tayari kufanya mazungumzo na kiongozi wa Azimio Raila Odinga.

“Rafiki yangu Raila Odinga, ninaenda Tanzania kwa mkutano unaongazia suala la rasilimali watu ili kuoanisha upanuzi wa fursa za ajira katika bara letu. Nitarudi kesho jioni, na kama ulivyokuwa ukijua, ninapatikana kukutana na wewe mmoja mmoja wakati wowote kwa urahisi,” Ruto aliandika.

Kauli yake ilikuja kama jibu la kiongozi wa upinzani Raila Odinga. Mnamo Jumanne tarehe 25 Julai, kiongozi wa Azimio la Umoja Raila Odinga alishutumu serikali ya Rais William Ruto kwa kukatisha juhudi za upatanishi za Rais wa Tanzania Samia Suluhu nchini.
Kupitia kwa kikao na wanahabari, Raila alifichua kuwa Rais Suluhu alizuru nchini majuma mawili yaliyopita lakini akakaa kusubiri kwa siku mbili.

Ziara ya Ruto Tanzania inajiri siku chache baada ya rais wa Tanzania kufichua kuwa baadhi ya wawekezaji walipiga kambi katika nchi hiyo jirani kutokana na kukosekana kwa utulivu wa kisiasa nchini Kenya. Katika video iliyosambazwa kwenye mitandao ya kijamii, Suluhu alibainisha kuwa serikali yake imekaribisha wawekezaji kadhaa ambao waliacha soko la Kenya kutokana na kukosekana kwa utulivu wa kisiasa.

Suluhu alisema maandamano dhidi ya serikali, ambayo yametikisa miji kadhaa ya Kenya, yalisababisha taharuki miongoni mwa wafanyabiashara wa kigeni.

Maoni yake hayakuwapendeza Wakenya wengi ambao wamemkosoa mkuu wa taifa wa Tanzania kwa kutowahi kuruka nafasi ya kulinganisha mataifa hayo mawili