Rais Ruto ametia saini Mswada wa Marekebisho ya Tume ya Uchaguzi IEBC 2024

Rais Kenya William Ruto leo Jumanne ametia saini kuwa sheria Mswada wa Marekebisho ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka, IEBC wa mwaka 2024.

Hafla hiyo imefanyika katika jumba la mikutano ya kimataifa la KICC jijini Nairobi.

 

Mswada huo ulipitishwa na bunge kufuatia mapendekezo yaliyowasilishwa na kamati ya uwiano wa kitaifa (NADCO) kwenye ripoti yake.

Sheria hiyo mpya italainisha utaratibu wa uchaguzi nchini na kutoa fursa ya kuapishwa kwa makamishna wapya wa IEBC.

Sheria ina miongoni mwa zingine jopo lililopanuliwa la kuajiri ambalo linajumuisha mwenyekiti na makamishna wa wakala wa uchaguzi.

Hafla hiyo fupi ilihudhuriwa na viongozi wa upinzani akiwemo Raila Odinga na Kalonzo Musyoka.

Viongozi wa upinzani na wale wa kidini wamekuwa wakitoa wito wa kutiwa saini kwa mswada huo ili kutoa fursa ya kuundwa upya kwa tume hiyo.