Tanzania yaidhinisha mradi wa bomba la mafuta wenye thamani ya dola bilioni 3.5

Rais wa Tanzania Samia Suluhu na Rais wa Uganda Yoweri Museveni

Serikali ya Tanzania ilitoa kibali chake siku ya Jumanne kwa ujenzi wa bomba la mafuta ghafi lenye thamani ya dola bilioni 3.5, sehemu ya mradi mkubwa wenye utata ambao umeibua wasiwasi juu ya haki za binadamu na mazingira.

Bomba hilo lenye urefu wa kilomita 1,443 litasafirisha mafuta ghafi kutoka kwenye maeneo makubwa ya mafuta yanayoendelezwa katika Ziwa Albert kaskazini magharibi mwa Uganda hadi bandari ya Tanzania kwenye Bahari ya Hindi.

Bomba hilo lilihitaji kibali kutoka kwa nchi zote mbili, na mwezi uliopita Uganda ilitoa leseni kwa mwendeshaji wa mradi huo, Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).

“Uidhinishaji huu wa ujenzi unaashiria hatua nyingine ya kusonga mbele kwa EACOP kwani inaruhusu kuanza kwa shughuli kuu za ujenzi nchini Tanzania, baada ya kukamilika kwa mchakato unaoendelea wa upatikanaji wa ardhi,” Mkurugenzi Mkuu wa EACOP Tanzania, Wendy Brown alisema katika hafla ya kupokea hati ya idhini.

Mradi wa mashamba ya mafuta na bomba wenye thamani ya dola bilioni 10 umekabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa wanaharakati wa haki na makundi ya mazingira ambayo yanasema unatishia mfumo wa ikolojia dhaifu wa eneo hilo na maisha ya makumi kwa maelfu ya watu.

Inatengenezwa kwa pamoja na Shirika la Kitaifa la Mafuta la China Offshore (CNOOC) na TotalEnergies ya Ufaransa, pamoja na Kampuni ya Kitaifa ya Mafuta ya Uganda inayomilikiwa na serikali.