Tanzania Yakanusha Tuhuma Ya kutoroshwa kwa Wanyamapori Hadi Umoja wa Falme Za Kiarabu

Mdhibiti wa viwanja vya ndege nchini Tanzania amekanusha kuruhusu utoroshwaji wa wanyamapori kutoka mbuga ya Serengeti hadi nchi ya Umoja wa Falme za Kiarabu, UAE.

Ametoa taarifa hizo baada ya kuibuka madai katika mitandao ya kijamii kuwa baadhi ya wanyama pori wanasafirishwa  kisiri siri kupitia ndege za mizigo kutoka Loliondo wilaya ya Ngorongoro karibu na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, hadi Umoja wa Falme za Kiarabu.

Vile vile Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA)imesema madai hayo ni porojo na uongo mtupu.

TCAA aidha imesema  kuwa uwanja wa ndege wa Loliondo si sehemu maalumu ya kuingia au kutoka.

“Mamlaka ina mfumo wa ufuatiliaji wa wakati halisi na safari zote za ndege za kimataifa huingia na kutoka kupitia viwanja maalum vya kuingia/kutoka kama vile Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Aman Abeid Karume (AAKIA),” ilisema katika taarifa.

Shirika hilo limesema taarifa hizo zinalenga kulichafulia nchi jina na taswira na kuwataka Watanzania kuzipuuza.