Vijana wa Gen Z Kenya waanzisha chama chao cha kisiasa

Vijana nchini Kenya wametambulisha chama kipya cha siasa kilichopewa jina la 47 Voices of Kenya Congress, ambacho tayari kimeingia rasmi kwenye uwanja wa siasa baada ya kusajiliwa rasmi.

Hiki ni kama sura mpya inayoibuka katika siasa za vijana wa Kenya maarufu kama Gen Z, kupitia chama hicho kilichodhamiria kuwakilisha sauti za jamii na makabila 47 ya nchi hiyo

Hatua hiyo inasababisha muundo mpya kwenye kile ambacho hadi sasa kimekuwa vuguvugu lisilo na kiongozi.

Kupitia kauli mbiu yake ‘sauti kila mahali’ chama hicho kipya cha kisiasa nchini Kenya, kinachoongozwa kabisa na vijana kimedhamiria kuangazia masuala na matarajio ya vijana nchini.

 

Kwa mujibu wa kaimu mwenyekiti wa chama hicho Wycliffe Kamanda chama chenyewe kimejengwa kwenye misingi ya ubunifu, uadilifu na ushirikishwaji wa kila Mkenya bila kuzingatia asili au eneo anakotoka kijana.

Wamepata usajili rasmi kutoka kwa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, na sasa, wako kwenye kampeni ya kitaifa  wakiwahimiza vijana kujiandikisha kama wapiga kura na kujihusisha kisiasa.

 

Lakini hatua hii inaleta mwelekeo mpya. Kuibuka kwa Gen Z kulifafanuliwa kama vuguvugu lisilo na viongozi, lililopangwa mtandaoni, na kuchochewa na hatua za kiraia za hiari.

 

Maandamano ya Gen Z ya Juni 25, ingawa yalikuwa na nguvu, pia yaligeuka kuwa ya uharibifu katika baadhi ya maeneo. Sasa, wengi wanajiuliza ikiwa kurasimisha harakati ya Gen Z kunaweza kuleta mwelekeo zaidi au kupunguza nguvu zake.

 

Wakati huo huo, baadhi ya viongozi wa upinzani wameonyesha kuunga mkono wimbi la vijana na kuutumia ushawishi wao.