Malawi yaomba chanjo zaidi kupambana na mlipuko wa kipindupindu

Kituo cha Matibabu ya Kipindupindu, kinachofadhiliwa na Unicef, Shirika la Msalaba Mwekundu la Malawi na Misaada ya Uingereza, kimepigwa picha katika Hospitali ya Bwaila iliyopo mjini Lilongwe, Malawi, Januari 25, 2018. – Malawi imekuwa ikikabiliwa na mlipuko wa kipindupindu tangu mwishoni mwa mwaka 2017 na UNICEF Malawi inafanya juhudi za kudhibiti mlipuko huo (Picha na AMOS GUMULIRA / AFP)

Malawi inauomba Umoja wa Mataifa kupata chanjo zaidi za kipindupindu, ikihofia mvua kubwa inaweza kuzidisha mlipuko wa ugonjwa huo unaosababishwa na maji ambao hadi sasa umesababisha vifo vya watu 128.

Taifa hilo la kusini mwa Afrika limerekodi visa 4,420 tangu mwezi Machi, mojawapo ya visa vyake vya juu zaidi kuwahi kuripotiwa katika kipindi cha muongo mmoja.

“Tumeomba chanjo zaidi,” mkurugenzi wa huduma za afya ya kinga katika wizara ya afya, Storm Kabuluzi alisema.

“Dozi za ziada zinahitajika kwa mikoa ya kati na kaskazini, ambako ugonjwa huo umeenea kutoka maeneo “yanayokabiliwa na kipindupindu” kusini, Kabuluzi aliongeza.

Idadi ya maambukizi imeongezeka karibu mara tatu tangu mwezi Agosti, kulingana na takwimu za serikali, na wilaya 24 kati ya 28 sasa zimeathirika.

“Cha muhimu ni kudhibiti mlipuko wa kipindupindu leo,” alisema Kabuluzi.

“Jambo zuri kwa kipindupindu ni kwamba tunaweza kutibu na unaweza kuzuia. Cha muhimu ni kushirikiana na jamii kuhamasisha usafi.”

Kipindupindu huambukizwa kutokana na vijidudu ambavyo kwa ujumla huambukizwa kupitia chakula au maji machafu.

Husababisha kuhara na kutapika, na inaweza kuwa hatari hasa kwa watoto wadogo.

Maji yaliyotakaswa na usafi wa mazingira ni muhimu kwa kuzuia maambukizi, kulingana na Shirika la Afya Duniani (WHO), ambalo wiki iliyopita lilionya kuwa Malawi “iko katika ukingo wa shida ya afya ya umma”.

Balozi wa afya ya jamii nchini Malawi, Maziko Matemba, ameonya kuwa msimu wa mvua ambao kwa kawaida huanza Novemba, unaweza kufanya mambo kuwa mabaya zaidi.

Msemaji wa wizara ya afya aliliambia gazeti moja nchini humo siku ya Alhamisi kwamba mlipuko huo umezikamata mamlaka “bila kujiandaa”

Klorini na dawa nyingine zinazohitajika kukabiliana na ugonjwa huo pia zina upungufu.

Kipindupindu kinaweza kutibiwa kwa urahisi na ‘Oral Rehydration Solution’, lakini visa vikali zaidi vinaweza kuhitaji maji ya ndani na dawa za kuzuia bakteria ‘antibiotics’, WHO inasema.

Duniani kote, ugonjwa huu huathiri kati ya watu milioni 1.3 na milioni nne kila mwaka na kusababisha hadi vifo 143,000.