Simbachawene: Serikali ilitumia bilioni 17 kwa waathirka wa mabomu Mbagala 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), nchini Tanzania, George Simbachawene amesema, serikali ya nchi hiyo imelipa kiasi cha shilingi  bilioni 17.46 kwa waathirika wa mlipuko wa mabomu yaliyotokea katika Kambi ya JWTZ KJ 671 Mbagala jijini Dar es Salaam mnamo Aprili 29, 2009.

Simbachawene ameyasema hayo leo bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la mbunge wa jimbo la Mbagala, Abdalah Chaurembo aliyetaka kufahamu kauli ya serikali juu ya mapunjo ya fidia kwa wananchi walioathirika na mlipuko wa mabomu jimboni kwake.

Waziri Simbachawene, amesema kiasi hicho kilicholipwa kwa wananchi 12,647 si fidia bali ni mkono wa pole kwa walioathiriwa na janga hilo na malipo hayo yalitolewa kwa awamu sita kuanzia mwaka 2009 hadi 2020.

“Vile vile, Serikali ilitoa kifuta machozi pamoja na kugharamia huduma za mazishi kwa familia 29 zilizopoteza wapendwa wao kutokana na milipuko hiyo ya mabomu,” ameeleza.

Amefafanua kuwa yanapotokea majanga yanayosababishwa na nguvu za asili, ugonjwa wa mlipuko na yanayofanana na hayo, serikali hailipi fidia bali hutoa kifuta machozi kwa waathirika.

Waziri Simbachawene amesema katika tukio hilo Serikali iligharamia huduma za mazishi kwa familia 29 zilizopoteza wapendwa wao kutokana na milipuko hiyo ya mabomu.

“Zoezi la kutoa mkono wa pole kwa waathirika lilisitishwa rasmi na Serikali mweziachi 2020 baada ya walengwa wote waliokusudiwa kujitokeza na kulipwa,” amesema Simbachawene.

Hata hivyo Waziri ameliambia Bunge kuwa bado kuna watu wanaodai kifuta machozi na wamekuwa wakifiatilia malalamiko yao kuhusu uhalali.