Tume:Katiba mpya, utekaji, utitiri wa kodi chanzo cha ghasia za Oktoba

Ripoti ya Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Oktoba 29, 2025 imeeleza kuwa ghasia zilizotokea wakati na baada ya uchaguzi mkuu nchini Tanzania zilitokana na mkusanyiko wa changamoto za muda mrefu zilizokuwa zikijengeka ndani ya jamii bila kushughulikiwa ipasavyo.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo ambayo imewasilishwa leo mbele ya Rais Samia Suluhu Hassan, sababu hizo zimeainishwa katika makundi matano makuu, yakihusisha masuala ya kisiasa, kiuchumi, kijamii, kiutawala na kimataifa.

Tume imebainisha kuwa miongoni mwa vyanzo vikuu vya ghasia hizo ni malalamiko ya kisiasa yaliyodumu kwa muda mrefu. Haya yanajumuisha wito wa kupatikana kwa Katiba Mpya, haja ya kuimarisha demokrasia ndani ya mfumo wa vyama vingi vya siasa, pamoja na migogoro ya ndani ya vyama.

Aidha, hoja kuhusu maboresho ya Tume Huru ya Uchaguzi na mfumo mzima wa uchaguzi zimetajwa kuwa sehemu ya msingi ya malalamiko yaliyokuwa yakitolewa na wadau mbalimbali.

Katika eneo la pili, ripoti imeeleza kuwa hali ngumu ya maisha, ukosefu wa ajira, pamoja na malalamiko kuhusu wingi wa kodi na mazingira yasiyo rafiki kwa biashara vilichangia kuongeza hali ya kutoridhika miongoni mwa wananchi.

Tume inaeleza kuwa changamoto hizi ziliweka mazingira yaliyochangia kuibuka kwa hasira na hatimaye ghasia, hususan katika kipindi cha uchaguzi.

Ripoti pia imegusia changamoto za kijamii, ikiwemo mmomonyoko wa maadili, madai ya utekaji na kupotea kwa watu, pamoja na tuhuma za ubadhirifu wa mali za umma.

Kwa mujibu wa takwimu za Jeshi la Polisi Tanzania, watu 758 waliripotiwa kupotea, kutekwa au kujiteka katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita. Kati yao, watu 113 walipatikana, huku mashauri manane yakiendelea kufanyiwa uchunguzi.

Hivyo, watu 445 bado hawajapatikana, jambo ambalo, kwa mujibu wa ripoti, linaongeza hofu na malalamiko ya wananchi kuhusu usalama wao.

Katika kipengele kingine, Tume imeeleza kuwa utendaji wa baadhi ya watendaji na watumishi wa umma, hususan katika ngazi za chini kama serikali za mitaa, umechangia hali hiyo. Wananchi wengi wamelalamikia kutosikilizwa au kuchelewa kutatuliwa kwa kero zao, hali iliyoongeza hisia za kutengwa na mfumo wa utawala.

Aidha, ripoti imegusia uwepo wa athari za kimataifa, ikieleza kuwa katika mazingira ya sasa ya kidunia, mataifa mbalimbali hutanguliza maslahi yao katika mahusiano ya kimataifa. Kwa mujibu wa Tume, hali hiyo inaweza kuchochea matumizi ya mbinu na mikakati mbalimbali ya kujipatia ushawishi katika nchi zinazoendelea, ikiwemo Tanzania.