CHADEMA yaweka msimamo wa kutoshiriki kongamano la TCD

Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa CHADEMA

Chama Kikuu cha upinzani nchini Tanzania chama cha Chadema, kimesema hakitashiriki kongamano la amani lililoandaliwa na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), kwa madai kuwa ni mtego wa kucheleweshwa kwenye agenda yao ya Katiba Mpya.

Msimamo huo umetolewa leo Machi18, 2022, jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe wakati akitoa maazimio ya kikao cha Kamati Kuu ya Chadema, kilichofanyika Machi 16 hadi usiku wa kuamkia Machi 17.

Mkutano huo wa kitaifa wa haki, amani na maridhiano umepangwa kufanyika Machi 30 na 31, 2022 jijini Dodoma, huku mgeni rasmi akitarajiwa kuwa ni Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.

TCD ambayo kwa sasa Mwenyekiti wake  Zitto Kabwe ni muunganiko wa vyama vitano vyenye wabunge bungeni na madiwani ambavyo, ni Chama Cha Mapinduzi (CCM), ACT-Wazalendo, NCCR-Mageuzi, Chama Cha Wananchi (CUF) na Chadema.

Mbowe amesema hawatashiriki kwani wakati wa maandalizi na msingi wa maridhiano yanajengwa na kubainisha kasoro zinazowafanya kufanyika kwa maridhiano tofauti na hapo hakutakuwa na tija.

“Kuhusu kongamano la TCD, tumeshauriana haya maridhian yanayozungumzwa na TCD sisi hatujashirki kuandaa, viongozi walipitia taarifa kwanza na tukapitia yaliyopangwa. Tumeangalia vizuri tukasema hapana, hatushirki sababu hatuoni nia njema ya kutibu kiu ya Watanzania kuhusu katiba ,” amesema Mbowe.

Aidha Mbowe amesema kuwa chama chake kitashiri mazungumzo yote wanayoyaona yana nia njema kwa mtazamo wao

“Chadema tumesema tutashiriki mazungumzo yote tunayoyaona yana nia njema kwa mtazamo wetu. Kwa mtazamo wetu kongamano linalopangwa Dodoma ajenda yake haizungumzii katiba mpya, inakwepa hoja ya katiba mpya.”

Pamoja na hayo Mbowe amesema chama cha Chadema hakitashiriki kongamano hilo, kwa kuwa baadhi ya wadau waliopangwa kutoa mada, walishiriki kuandaa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020, akiwemo Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa (NEC), Dk. Wilson Mahera ambaye atatoa mada.

“Miongoni mwa wawasilisha mada ni mtu anaitwa Mahera, mkurugenzi wa uchaguzi, huyo ndiyo akatuhubirie maridhiano? Tunapaswa kukaa kwanza na tuangalie tatizo liko wapi ndio twesonge mbele. Kwa hiyo sisi hatutakwenda,” amesema Mbowe