King’ora cha tahadhari ya mashambulizi ya anga nchini Israel

King’ora cha tahadhari ya mashambulizi ya anga kimelia katika maeneo mbalimbali ya Israel, ikiwemo kitovu cha biashara cha Tel Aviv na mji wa pwani wa kusini wa Ashdod, kufuatia mashambulizi ya makombora kutoka Lebanon.

Hakukuwa na taarifa za haraka kuhusu vifo au majeruhi, lakini vyombo vya habari vya Israel viliripoti kuwa mifumo ya ulinzi wa anga ilifanikiwa kudungua angalau kombora moja lililokuwa linaelekea nchini humo.

Mapema leo Ijumaa, kundi la Hezbollah lilisema lilikuwa limeanzisha mawimbi matatu ya mashambulizi ya makombora na droni dhidi ya wanajeshi wa Israel pande zote za mpaka pamoja na mji mmoja kaskazini mwa Israel.

– Kiongozi wa Iran atoa ujumbe mpya kwa maandishi –

Kiongozi mpya wa juu wa Iran, Mojtaba Khamenei, alisema katika ujumbe wake wa hivi karibuni wa maandishi kuwa Jamhuri ya Kiislamu haitaki vita na Marekani na Israel, lakini italinda haki zake kama taifa, kwa mujibu wa televisheni ya taifa.

“Hatutakataa haki zetu halali chini ya hali yoyote ile, na kwa mtazamo huu, tunaichukulia kambi nzima ya mapambano ya upinzani kama kitu kimoja,” aliongeza, akimaanisha Lebanon, ambako Israel inapigana na mshirika wa Tehran, Hezbollah.

Khamenei bado hajaonekana hadharani tangu alipoteuliwa kumrithi baba yake, ambaye aliuawa katika wimbi la kwanza la mashambulizi tarehe 28 Februari.

– Trump asema Iran inafanya kazi ‘mbaya sana’ kuhusu Hormuz –

Rais wa Marekani Donald Trump aliishutumu Iran kwa kufanya “kazi mbaya sana” katika kuruhusu mafuta kupita kupitia Mlango wa Bahari wa Hormuz na kwa kukiuka makubaliano ya kusitisha mapigano ya muda ya wiki mbili.

“Iran inafanya kazi mbaya sana, wengine wanaweza kusema kwa aibu, katika kuruhusu mafuta kupita katika Mlango wa Hormuz,” alisema Trump kupitia jukwaa lake la Truth Social. “Hiyo si makubaliano tuliyofikia!”

Trump pia aliionya Iran dhidi ya kutoza ushuru kwa meli zinazopita katika Mlango wa Hormuz.

“Kuna taarifa kuwa Iran inatoza ada kwa meli za mafuta zinazopita katika Mlango wa Hormuz ni heri isiwe hivyo, na kama ni kweli, basi waache mara moja!” alisema kupitia Truth Social.

Katika ujumbe mwingine dakika chache baadaye, Trump aliongeza kuwa “kwa haraka sana, utaona mafuta yakianza kupita, kwa msaada wa Iran au bila msaada wao.”

– Israel yatoa amri ya kuhama kwa wakazi wa Beirut –

Jeshi la Israel liliwaonya wakazi wa vitongoji vya kusini mwa Beirut, ambavyo kwa muda mrefu vimekuwa ngome ya kundi la Hezbollah, kuhusu mashambulizi yanayokaribia na kuwataka wahame.

Shirika la Afya Duniani (WHO) lilihimiza Israel kufuta amri hiyo ya kuhama, likisema eneo hilo lina hospitali mbili.

Tangazo hilo lilikuja siku moja baada ya Israel kufanya wimbi kubwa zaidi la mashambulizi tangu kuanza kwa vita vyake na Hezbollah tarehe 2 Machi, ambapo zaidi ya watu 300 waliuawa na zaidi ya 1,000 kujeruhiwa, kulingana na wizara ya afya ya Lebanon.

Wakati Israel ikitoa agizo hilo kwa raia wake, Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer na Trump walitoa wito wa kuwa na “mpango wa vitendo” ili kurejesha usafirishaji wa meli katika Mlango wa Hormuz baada ya kusitishwa kwa mapigano kati ya Marekani na Iran, ofisi ya kiongozi huyo wa Uingereza ilisema.

Viongozi hao wawili “walikubaliana kuwa sasa kuna usitishaji wa mapigano na makubaliano ya kufungua mlango huo, hatua inayofuata ni kutafuta suluhisho,” kulingana na Downing Street.

“Viongozi walijadili umuhimu wa kuwa na mpango wa vitendo ili kurejesha haraka usafirishaji wa meli,” na walikubaliana kuzungumza tena.

– Maombolezo ya Khamenei –

Maelfu ya Wairani walikusanyika kuomboleza aliyekuwa kiongozi wa juu Ali Khamenei, aliyeuawa siku ya kwanza ya vita.

Wakiwa wamebeba picha za kiongozi wao marehemu na kupeperusha bendera ya Jamhuri ya Kiislamu, wafuasi wa Khamenei walishiriki maandamano kote nchini baada ya kifo chake katika shambulio la pamoja la Marekani na Israel tarehe 28 Februari.