Mahakama yahalalisha mkataba wa bandari, walalamikaji kupinga uamuzi huo mahakama ya rufaa.

Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya hii leo imetoa uamuzi kuwa mkataba wa IGA baina ya Serikali ya Tanzania na ile ya Dubai hauna tatizo na ni halali hivyo pingamizi lililowekwa na walalamikaji halina mashiko. 

Uamuzi huo umesomwa na jopo la majaji watatu likiongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru, akishirikiana na majaji Mustafa Ismail na Abdi Kagomba. 

Katika vilivyotolewa uamuzi na mahakama ni pamoja na: Kama ibara ya 2, 4(2)… zinakiuka Ibara namba 1, 8 na 28(1) na (3) za Katiba ya nchi na pia kama IGA ni mkataba kwa muktadha wa Sheria ya Mikataba.Katika viini hivyo Mahakama imesema IGA si mkataba unaoweza kusimamiwa na sheria ya mkataba. 

“Mahakama imekubali kuwa Dubai ina mamlaka ya kuingia mikataba kama huo. Walalamikaji hawajaeleza kama Dubai imezuiliwa kuingia mkataba wa ushirikiano wa uwekezaji kwani ni suala la ushahidi. Nakubaliana na Wakili wa Serikali kuwa aina uwezo wa kuingia mikataba ya ushirikiano wa kiuwekezaji,”amesema Jaji Ndunguru. 

Kuhusu kama IGA inakiuka kifungu cha 64 cha Sheria ya Manunuzi, Mahakama imesema; “Mahakama imeikataa hoja hiyo ikisema IGA ni mkataba wa kimataifa na kwamba katika mkataba huo hakuna manunuzi yaliyofanyika. Kama walalamikaji wakiona TPA (Mamlaka ya Bandari) iliingia katika manunuzi basi walipaswa kuinganisha TPA katika kesi hii, kwa hiyo hoja nayo Mahakama imeikataa.”

Nje ya mahakama mara baada ya kusomwa kwa hukumu hiyo, walalamikaji katika kesi hiyo wamesema wanajipanga kukata rufaa kuupinga uamuzi huo kutokana na kutoridhiswa nao.

“Kwa kuwa Mahakama imesema haina mamlaka ya kuingilia shughuli za Bunge sasa sisi tunakwenda kutumia Civil Bunge (Bunge la Wananchi) tutatoa siku 14 wabadiki mkataba huu,” amesema Wakili Boniface Mwabukusi

Sakata la uwekezaji bandari kati ya Serikali ya Tanzania na Dubai kupitia kampuni ya DP World kwa mara ya kwanza lilifika mahakamani jijini Mbeya Julai 3,2023

Kesi hiyo iliongozwa na mawakili Boniface Mwabukusi na Philipo Mwakilima, ilifunguliwa kupinga baadhi ya vifungu vya mkataba huo.

Kesi hiyo namba 05/2023 iliwahusisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na Katibu wa Bunge.