Mbunge wa CCM afariki dunia

Mbunge wa Aman (CCM), Mussa Hassan Mussa amefariki dunia leo Alhamisi Oktoba 13, 2022 nyumbani kwake visiwani Zanzibar.

Akitoa taarifa ya kifo hicho leo Alhamisi Oktoba 13, 2022 Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson amesema ofisi ya bunge kwa kushirikiana na familia inaratibu mipango ya mazishi.

“ Nimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha Mhe. Mussa Hassan Mussa, natoa pole kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa, waheshimiwa wabunge na wananchi wa Jimbo la Amani. Mwenyezi Mungu awape moyo wa uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu” imeeleza taarifa hiyo iliyotolewa na Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano wa Kimataifa, Ofisi ya Bunge imeeleza kuwa Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson ametangaza kifo hicho.

Kifo cha Mussa (63) kinafikisha idadi ya Wabunge saba ambao wamefariki dunia hadi sasa ambao kati yao watano ni wabunge wa majimbo na wawili wa Viti Maalum.

Wabunge wengine waliofariki katika bunge la 12 ni Atashasta Nditiye (Muhambwe), Eliasi Kwandikwa (Ushetu), William Ole Nasha (Ngorongoro), Said Khatibu Haji (Konde), Martha Jachi Umbula na Irene Ndyamukama waliokuwa wa Viti Maalum.