Mgomo wa usafiri Kenya kutokana na kupanda kwa bei ya mafuta waingia siku ya pili

 

 

 

Mgomo wa sekta ya usafiri nchini Kenya, uliosababishwa na vita vya Mashariki ya Kati, uliifanya nchi kusimama kwa siku ya pili mfululizo leo Jumanne baada ya watu wanne kufariki na makumi ya wengine kujeruhiwa siku ya jana Mei 18,2026.

Kenya, ambayo ni miongoni mwa nchi nyingi za Afrika zinazotegemea uagizaji wa mafuta kutoka Ghuba ya Uajemi, imeongeza bei ya petroli kwa asilimia 20 na dizeli kwa karibu asilimia 50 tangu Iran ilipozuia usafiri kupitia Mlango wa Bahari wa Hormuz, ambapo kwa kawaida hupita takribani sehemu ya tano ya mafuta yote duniani.

Sekta ya usafiri, hasa waendeshaji wa mabasi ya “matatu” ambayo hutoa huduma kubwa ya usafiri wa umma nchini Kenya, ilitangaza mgomo huo baada ya ongezeko jingine kubwa la bei wiki iliyopita.

Waendeshaji wa matatu walishindwa kufikia makubaliano ya kupunguza bei katika mazungumzo na serikali siku ya jana Jumatatu, hali iliyosababisha mgomo huo kuendelea.

Barabara za Nairobi zilionekana karibu tupu tena mapema Jumanne, huku kukiwa na taarifa kwamba vijana walikuwa wakizuia tena barabara kuu zinazoingia katika mji mkuu pamoja na maeneo ya miji mingine kama Naivasha.

Shule ziliendelea kufungwa kwa siku ya pili jijini Nairobi huku balozi kadhaa zikitangaza kufungwa kutokana na mgomo huo unaoendelea.

Waziri wa Mambo ya Ndani Kipchumba Murkomen aliwaambia waandishi wa habari Jumatatu kuwa watu wanne waliuawa na zaidi ya watu 30 kujeruhiwa katika vurugu zilizohusishwa na maandamano hayo yaliyofanyika kote nchini.

Kundi la kutetea haki za binadamu nchini Kenya, Vocal Africa, lililaani “matumizi ya nguvu za mauaji na vyombo vya sheria”.

Waziri wa Mipango ya Uchumi, John Mbadi, alisema mgomo huo “haukuwa na sababu yoyote ya msingi”.

“Hii ni vita ambavyo hatukuvianzisha,” alisema kupitia kituo cha televisheni cha NTV Jumatatu.

Wakosoaji wanasema Kenya ina ushuru mkubwa wa mafuta ambao unaweza kupunguzwa, ingawa serikali pia inategemea mapato hayo kuhudumia deni kubwa la taifa na bajeti yenye changamoto.

Mamlaka ya kudhibiti sekta ya nishati ilisema wiki iliyopita kuwa serikali ilikuwa imetumia dola milioni 38.5 kuwasaidia walaji kukabiliana na ongezeko la bei ya dizeli na mafuta ya taa.

Mwezi uliopita, mamlaka za Kenya pia zilisimamisha viwango vya ubora wa mafuta ili kuhakikisha upatikanaji wake wakati wa uhaba.

Ingawa Kenya ni miongoni mwa uchumi wenye kasi kubwa ya ukuaji Afrika Mashariki, takribani theluthi moja ya wananchi wake milioni 50 bado wanaishi katika umaskini.