Mradi wa visima vya maji kupunguza adha ya upatikanaji maji Dar

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa leo Novemba 2 amezindua mradi wa maji Kigamboni utakaozalisha lita milioni 70 na kusaidia kuondoa adha ya maji katika wilaya ya Kigamboni na baadhi ya maeneo ya katikati ya jiji.

Mradi huo unahusisha visima saba na tenki la kuhifadhia maji lenye ukubwa la lita 15 milioni unatekelezwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira (Dawasa) umekamilika kipindi ambacho jiji la Dar es Salaam lina uhaba mkubwa wa maji.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Waziri Mkuu Majaliwa amesema lita hizo milioni 70 zitaungana na lita 300 milioni zinazozalishwa kwa sasa na chanzo cha maji cha mto Ruvu ambacho bado hakikidhi mahitaji.

Kwa mujibu wa Waziri Mkuu ni kwamba matumizi ya maji kwa mkoa wa Dar es Salaam kwa siku ni lita 540 milioni na mto Ruvu unazalisha lita 520 milioni lakini katika kipindi hiki cha ukame maji yanayopatikana kwenye chanzo hicho ni lita 300 milioni pekee.

Kufuatia hilo Waziri Mkuu ametoa maelekezo ya kuchimbwa kwa visima vingine Kigamboni kwa kuwa ni eneo ambalo limethibitika kitaalam kuwa lina maji ya kutosha chini ya ardhi.

Pia Waziri Mkuu ameagiza maji hayo yasiishie Kigamboni na Temeke bali yapelekwe pia Ubungo, Sinza na Kinondoni ambapo pia kuna adha kubwa ya upatikanaji wa maji.