Mwili wa Mwanzilishi wa Precision Air kuzikwa leo

Mwili wa Mwanzilishi na Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Shirika la Ndege la Precision Air, Michael Ngaleku Shirima unatarajiwa kuzikwa leo  katika makaburi ya familia katika Kijiji cha Nayeme, Tarakea, Wilaya ya Rombo, mkoani Kilimanjaro.

Mzee Ngaleku alifariki usiku wa Juni 9, mwaka huu katika Hospitali ya Aghakan, Dar es salama alikokuwa amelezwa Juni 8

Mwili huo umewasili kijijini kwake jana jioni na ulipokelewa na mamia ya wananchi wakiwemo wafanyabiashara mashuhuri wa Mkoa wa Kilimanjaro, watawa wa kanisa Katoliki ambao wanahudumu katika kituo cha  kulelea watoto yatima cha Ngaleku kituo ambacho alikijenga Mzee Ngaleku pamoja na  viongozi wa chama na serikali wa mkoa huo.

Hata hivyo mwili wa mfanyabiashara huyo nguli wa  anga, umesindikizwa na viongozi mbalimbali wa serikali kutokea Jijini Arusha akiwemo Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia na Mbunge wa Rombo, Profesa Adolf Mkenda, baadhi ya wabunge wa Bunge la Tanzania, wafanyabiashara mashuhuri nje na ndani ya Mkoa wa  Kilimanjaro pamoja na viongozi wengine waliokuwepo katika msafara huo.