Nisamehe- Jenerali Muhoozi amwambia Rais Ruto                                

Mtoto wa rais wa Uganda Yoweri Museveni ameomba msamaha kufuatia mitandao ya kijamii iliyojumuisha tishio la kuvamia nchi jirani ya Kenya.

Matamshi hayo yaliyotumwa kwenye mtandao wa Twitter mwezi huu na Jenerali Muhoozi Kainerugaba mwenye umri wa miaka 48, yalisababisha hasira nchini Kenya na miito ya hasira ya kutaka maelezo rasmi kutoka Uganda.

“Sijawahi kuwa na tatizo lolote na Afande Ruto,” Kainerugaba aliandika kwenye ukurasa wake wa Twitter Alhamisi jioni, akimaanisha Rais mpya wa Kenya William Ruto.

“Kama nilifanya makosa mahali popote, namuomba anisamehe kama mdogo wake.”

Miongoni mwa matamshi mengine, Kainerugaba alipendekeza kuchukua wanajeshi wake kuteka Nairobi na kumkashifu kiongozi wa zamani wa Kenya Uhuru Kenyatta kwa kutojaribu kugombea nafasi ya tatu kinyume cha katiba katika uchaguzi wa Agosti.

Sio mara ya kwanza kwa kauli ya Kainerugaba kuhusu masuala nyeti ya sera za kigeni kusababisha maumivu ya kidiplomasia kwa Uganda, na Museveni mwenyewe alitoa taarifa wiki iliyopita akitaka msamaha wa Kenya.

Museveni, ambaye alikuwa amehudhuria hafla ya kuapishwa kwa Ruto mwezi uliopita, alimkemea mwanawe kwa “kuingilia masuala” ya Kenya na kuzungumza hadharani kuhusu masuala ya kisiasa, jambo ambalo anazuiwa kufanya kama afisa wa ngazi ya juu wa jeshi.

Kiongozi huyo aliyehudumu kwa muda mrefu nchini Uganda pia alitangaza kuwa Kainerugaba hataongoza tena vikosi vya ardhini vya nchi hiyo, ingawa alipandishwa cheo na kuwa jenerali.

Ujumbe wa Kainerugaba wa kuunga mkono waasi wa Tigray kaskazini mwa Ethiopia uliikasirisha Addis Ababa, huku mawazo yake juu ya uvamizi wa Urusi nchini Ukraine na mapinduzi ya mwaka jana nchini Guinea pia yakiibua hisia kali.