Polisi nchini Msumbuji watumia mabomu ya machozi kuwatawanya waandamanaji

Polisi nchini Msumbiji walitumia gesi ya kutoa machozi leo Jumatatu kutawanya umati mdogo katika mji wa Maputo, ambapo maduka yalikuwa yamefungwa kabla ya maandamano yaliyoandaliwa kupinga udanganyifu wa uchaguzi. 

Kulingana na video zilizopostiwa kwenye mitandao ya kijamii watu kadhaa, wakiwemo waandishi wa habari, walikimbia baada ya polisi waliovaa silaha nzito kutembea kwenye barabara kuu.

Kiongozi wa upinzani, Venancio Mondlane, ambaye aligombea urais katika uchaguzi wa tarehe 9 Oktoba, alitangaza maandamano hayo kupinga matokeo ya awali yanayoonyesha kwamba chama tawala cha Frelimo kimepata ushindi. 

Matarajio yaliongezeka baada ya washirika wawili wa Mondlane kuuawa kwa risasi siku ya Jumamosi. Mwanasheria Elvino Dias na Paulo Guambe, mgombea kutoka chama kidogo cha Podemos kinachomuunga mkono Mondlane, walikuwapo kwenye gari ambalo lilizingirwa na magari mengine kisha wakapigwa risasi, walieleza mashahidi.

Kiongozi wa Podemos, Albino Forquilha, alithibitisha mauaji hayo huku polisi wakisema uchunguzi umeanzishwa lakini hawakuthibitisha majina ya wanaume hao wawili.

Muungano wa Ulaya, Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa wamedai kukatishwa tamaa na tukio hilo na kuwataka mamlaka kubaini wahusika. Katika taarifa, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, aliwataka “Wamozambiki wote, wakiwemo viongozi wa kisiasa na wafuasi wao, kubaki watulivu, kujizuia na kukataa aina zote za vurugu.”

Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, Moussa Faki Mahamat, alisema ana “huzuni kubwa” kuhusu “matukio yaliyoripotiwa ya vurugu baada ya uchaguzi, hasa mauaji ya hivi karibuni.”

Maputo ilikuwa kama mji wa mzimu siku ya Jumatatu, huku maduka yakiwa yamefungwa na helikopta zikifanya doria juu ya jiji lenye watu wapatao milioni moja. 

Msumbiji, ambayo inasubiri matokeo rasmi ya urais na bunge wiki hii, imeshuhudia vurugu za uchaguzi hapo awali. Mwaka jana, watu kadhaa waliuawa katika mapambano baada ya uchaguzi wa mitaa.