Watatu wadaiwa kumbaka mwanafunzi mkoani Shinyanga

Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga linawashikilia vijana watatu kwa tuhuma za kumbaka mwanafunzi wa shule ya sekondari Kishimba iliyopo Manispaa ya Kahama mkoani humo wakati akitoka dukani kununua vitu.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Janeth Magomi amesema tukio hilo limetokea Julai 8, mwaka huu katika Kijiji cha Igumhwa Kata ya Kitwana Wilaya ya Kahama saa saba mchana wakati binti huyo (14) alipokuwa akitoka dukani ndipo walimshika na kumbaka.

Amewataja vijana hao ni Dotto Venancy (18), Juma Mwita (17) na Paul Peter (17) ambao walihusika kumvamia binti huyo alipokuwa akielekea nyumbani na kisha kumfanyia kitendo hicho cha kikatili.

Kamanda Magomi amesema jeshi hilo linaendelea kumsaka mtuhumiwa mmoja aliyetoroka baada ya kufanya kitendo hicho.