Wizara ya Maji Tanzania yaomba bajeti ya bilioni 709.36 kwa matumizi ya wizara hiyo

Waziri  wa Maji Tanzania, Jumaa Aweso

Waziri  wa Maji Jumaa Aweso, ameliomba Bunge limuidhinishie jumla ya Shilingi Billioni 709.36 kwa ajili ya matumizi ya Wizara ya Maji kwa mwaka 2022/23.

Kati ya fedha hizo, matumizi ya kawaida ni Shilingi Billioni 51.46 ambapo Shilingi Billioni 16.7 sawa na asilimia 32.45 ni kwa ajili ya kugharamia matumizi mengineyo (OC) na Shilingi Billioni 34.7 sawa na asilimia 67.55 ni kwa ajili ya kulipa mishahara (PE) ya watumishi wa Wizara, RUWASA na Chuo cha Maji.

Jumla ya bajeti ya maendeleo ni Shilingi Billioni 657.8 ambapo kati ya fedha hizo, Shilingi Billioni 407.06 sawa na asilimia 61.87 ni fedha za ndani na Shilingi  Billioni 250.8 sawa na asilimia 38.13 ni fedha za nje.

Amesema Wizara kupitia maabara 17 za kupima ubora wa maji nchini, zimeendelea kuhakiki na kufuatilia ubora wa maji kwenye vyanzo vya maji na mitandao ya kusambaza maji mijini na vijijini.

“Nchi yetu haina uhaba wa maji hata hivyo Serikali inaendelea kuwekeza katika vyanzo vyama vya maji ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya kuwezesha upatikanaji wa maji, kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi na kuboresha ufanisi katika matumizi ya maji.” Amesema Aweso

Amesema katika kuhakikisha upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama vijijini mwaka 2025, Serikali imeendelea kujenga, kukarabati na kuimarisha usimamizi wa huduma za maji vijijini

“Serikali imeendelea kuboresha hali ya upatikanaji wa huduma ya maji katika Jiji la Dodoma ambapo Wizara imekamilisha utekelezaji wa miradi ya kutoa maji katika visima vya Ihumwa kwenda tanki la Njedengwa; mradi wa kuboresha hali ya upatikanaji wa majisafi Chamwino –Ikulu.”Amesema

Aidha amesema Wizara inaendelea na utekelezaji wa mradi wa kuchimba visima vipya na kukarabati visima vya zamani

Pia amesema katika jitihada za kukabiliana na uhaba wa huduma ya maji katika jiji la Dodoma, Serikali imepata mkopo wa Dola za Marekani milioni 125.3 kutoka Benki ya Maendeleo Africa (AfDB) kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Bwawa la Farkwa na mtambo wa kutibu maji ambapo ujenzi unatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2022/23.

“Katika kuhakikisha kuwa upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama kwa wananchi waishio vijijini inafikia zaidi ya asilimia 85 ifikapo mwaka 2025, Serikali imeendelea kujenga, kukarabati, kupanua mitandao ya kusambaza maji pamoja na kuimarisha usimamizi wa huduma ya maji.

“Hadi kufikia mwezi Aprili 2022, upatikanaji wa huduma ya maji vijijini imefikia wastani wa asilimia 74.5 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 72.3 mwezi Machi, 2021.

Amesema kiwango hicho kinatokana na kukamilika kwa ujenzi wa miradi mipya, ukarabati na upanuzi wa miradi 303 ambayo imeanza kutoa huduma kwa zaidi ya wananchi 1,467,107