Washtakiwa 23 ambao ni viongozi na wanachama wa Chama cha Demokrsia na Maendeleo Chadema Jijini Mwanza wamepandishwa kizimbani katika Mahakama Kuu ya Mwanza kwa kosa la kupanga kufanya vitendo vya kigaidi.

Akisoma shitaka hilo namba1637/2026 Mwendesha mashitaka mkuu wa serikali wakili Maugo amesema washtakiwa hao kati ya tarehe tofauti kuanzia Juni 25-Julai 6,2026 kwa nyakati tofauti katika wilaya za Ilemela na Nyamagana walishiriki kwenye vikao vya kigaidi wakipanga njama za kuchoma na kuharibu majengo na miundombinu ya serikali na watu binafsi mpango uliotarajiwa kufanyika Julai 7,2026.
Wakili wa serikali Maugo amesema washtakiwa hao wametenda kosa hilo kinyume na kifungu cha 4(i na ii) kifungu cha 5, kifungu cha 12, kifungu cha sheria ya kuzia ugaidi pamoja na kifungu cha 57 cha sheria ya uhujumu uchumi.
Katika kesi hiyo wakili Maugo anashirikiana na Janes Kiwelo wakili mwandamizi wa serikali pamoja na Silelo Mazura wakili wa serikali
Akizungumza nje ya Mahakama wakili upande wa washtakiwa Erick Mutta amesema washtakiwa hao walishitakiwa kwa kesi mbili tofauti ikiwemo hiyo ya kupanga njama za kupanga kufanya vitendo vya kigaidi wakiwa na lengo la kuchoma majengo ya serikali au kulipua.
Amesema mahakama hiyo haina uwezo wa kusikiliza kesi hiyo hivyo wamerudishwa rumande mpaka tarehe 6/8/2026 itakapokuja kwa ajili ya kutajwa.
Katibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema Zacharia Obadi ameiomba serikali kuacha tabia ya kutengeneza kesi zenye lengo la kuwaumiza wananchi.