Mamia ya watu nchini Japan wamefanikiwa kufunga ndoa baada ya kukutana kupitia programu ya kutafuta wapenzi inayotumia akili bandia (AI), iliyozinduliwa na Serikali ya Jiji la Tokyo mwaka 2024 ikiwa ni sehemu ya juhudi za kukabiliana na kiwango cha chini cha uzazi nchini humo.
Kwa mujibu wa takwimu za serikali zilizotolewa mwezi huu, jumla ya wanandoa 265 wamefunga ndoa baada ya kukutana kupitia programu hiyo inayojulikana kama TOKYO Enmusubi.
Programu hiyo ilianza kutumika mwezi Septemba 2024 kufuatia utafiti ulioonyesha kuwa takribani asilimia 70 ya watu waliotamani kuoa au kuolewa hawakuwa wakishiriki kikamilifu katika shughuli za kutafuta wenza.
Ili kuhakikisha wanaojiunga wana dhamira ya kweli ya kufunga ndoa, waombaji walitakiwa kuthibitisha kuwa hawajaoa au kuolewa kisheria, pamoja na kufaulu mahojiano yaliyofanyika mtandaoni kabla ya kukubaliwa.
Hadi Juni 30 mwaka huu, programu hiyo ilikuwa na wanachama 16,000 waliokubaliwa kati ya waombaji karibu 36,000. Kati yao, wanandoa 760 walikuwa katika mahusiano ya dhati, huku 265 tayari wakiwa wamefunga ndoa.
Mwanamke mmoja aliyefahamishwa kwa jina la utani la “Turtle” alisema aliamua kujiunga na programu hiyo kama fursa yake ya mwisho alipokuwa akikaribia kutimiza miaka 40.
Alisema baada ya kukutana na watu kadhaa kupitia miadi ya utambulisho, alikutana na mwanaume ambaye baadaye alikuja kuwa mume wake mwishoni mwa Agosti, wakaanza uhusiano wa dhati katikati ya Septemba, na akakubali ombi la ndoa mwishoni mwa Desemba.
Japan inaendelea kukabiliwa na changamoto ya kupungua kwa idadi ya watoto wanaozaliwa. Takwimu za Wizara ya Afya, Kazi na Ustawi wa Jamii zinaonyesha kuwa mwaka 2025 watoto 671,236 pekee walizaliwa na raia wa Japan, kiwango cha chini zaidi kuwahi kurekodiwa na mwaka wa 10 mfululizo wa kupungua kwa idadi ya vizazi.
Katika kipindi hicho, vifo vilifikia zaidi ya milioni 1.6, huku kiwango cha uzazi kikishuka hadi watoto 1.14 kwa mwanamke mmoja, licha ya ongezeko dogo la idadi ya ndoa.
Mtumiaji mwingine wa programu hiyo, aliyefahamishwa kwa jina la “Skytree”, alisema mfumo wa AI ulisaidia kuwapa ujasiri wa kukutana na watu waliopendekezwa kwa kuonyesha kiwango cha ulinganifu wao katika hatua tatu.
“AI ilionyesha kuwa mimi na mpenzi wangu tulikuwa na ulinganifu wa asilimia kamili, jambo lililonipa imani ya kuendelea na uhusiano,” alisema.