Maduka ya dawa binafsi yaliyo nje ya hospitali za Serikali kuondolewa

Imeelezwa kwamba maduka hayo yapo kinyume cha kanuni ya Famasia

0
Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya

Wizara ya Afya nchini Tanzania imewaagiza wamiliki wote wa maduka ya dawa yaliyopo mita 500 kutoka vituo vya afya nchini kuyaondoa ifikapo Juni 30 mwaka huu.

Kwa mujibu wa Wizara hiyo  maduka hayo yapo kinyume cha kanuni ya famasia iliyowekwa mwaka 2020 hivyo wamiliki watachukuliwa hatua za kisheria.

Akizungumza leo  na wanahabari akiwa hospitali ya Taifa Muhimbili-Upanga kwa lengo la kuangalia ubora wa utoaji huduma kwa wagonjwa.Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema muda ulishatolewa wa kutosha na jambo hilo halipaswi kuendelea kwa kuwa ni kinyume na sheria.

“Ninatuma salamu maduka yote ya dawa lazima yawe mita 500 kutoka ndani ya hospitali, tunakwenda kuyaondoa ifikapo Julai Mosi mwaka huu tulishatoa muda wa kutosha kufikia Juni 30 yawe yameondoka.

“Wamiliki wanafanya kinyume cha sheria nipo na mfamasia Mkuu wa serikali hapa, tulitunga na tulipitisha kanuni maduka yote yawe mita 500 kutoka hospitalini nikaambiwa waziri kuna wengine walipewa leseni kabla, hivyo tumebakisha miezi mitano hakuna cha msalie mtume wala kuomba radhi,” amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy ameyasema hayo baada ya kukutana na malalamiko ya ukosefu wa dawa kutoka kwa wagonjwa hospitalini hapo.

“Mwananchi anakosaje dawa? Suala hili ni la pande mbili MSD na hospitali na nilishatoa maagizo. Uwepo wa haya maduka yanachangia udokozi wa dawa na yanaondoa imani kwa wananchi kwamba angalau kuna usimamizi mzuri wa dawa vituoni,” amesema.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted