Watoto wa familia moja wafariki kwa kukosa hewa

Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia jana Jumapili, ambapo chanzo kimetajwa kuwa ni moto wa mkaa uliokuwa umewashwa ndani ili kuwapa joto watoto hao.

0
Kamanda wa Polisi Mkoani Tabora,  Richard Abwao

Watoto wawili wa familia moja wamefariki dunia baada ya kukosa hewa wakiwa katika nyumba waliyokuwa wamelala katika Kijiji cha Usubilo kata ya Ifucha halmashauri ya Manispaa ya Tabora. 

Kamanda wa Polisi Mkoani Tabora,  Richard Abwao amewataja watoto waliofariki kuwa ni  Amani Athuman mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi sita na Zainabu Athumani mwenye umri wa mwaka mmoja.

Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia jana Jumapili, ambapo  chanzo kimetajwa kuwa ni moto wa mkaa uliokuwa umewashwa ndani ili kuwapa joto watoto hao kutokana na baridi kali kipindi hiki cha mvua.

Kamanda Abwao ameeleza kuwa moshi wa moto huo ulipelekea watoto hao waliokuwa wamelala kukosa hewa ya kutosha kutokana na sehemu ndogo ya kupitisha hewa katika nyumba hiyo.

“Kutokana na miundombinu isiyoridhisha ya madirisha kuwa madogo, kulisababisha watoto kukosa hewa ya kutosha” amesema Kamanda Abwao

Kamanda amesema kuwa moshi huo umewaathiri baba mzazi wa watoto hao, Athuman Shaban (45) mkewe Magreth Joseph (34) pamoja na binti yao Neema Athumani (17) ambao wamelazwa katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa (Kitete).

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted