Dkt Jafo asema samaki wa Ziwa Victoria hawajaathirika kwa Zebaki

Amesema wataalamu wanaendelea kuhakikisha matumizi mbalimbali ya kemikali hiyo katika maeneo ya Kanda ya Ziwa yanadhibitiwa

0
Dkt. Selemani Jafo,Waziri wa Nchin Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira)

Waziri wa Nchin Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Selemani Jafo amesema tafiti zinaonesha samaki na dagaa wanaopatikana katika Ziwa Victoria hawajaathirika kwa madini ya zebaki.

Dkt. Jafo ameyasema hayo bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Juliana Masaburi aliyetaka kufahamu iwapo Serikali imefanya utafiti kuhusu samaki hao iwapo wameathiriwa na kemikali hiyo kama inavyodaiwa.

Dkt. Jafo alisema kuwa wataalamu wanaendelea kuhakikisha matumizi mbalimbali ya kemikali hiyo katika maeneo ya Kanda ya Ziwa yanadhibitiwa huku akiwataka waendelee kuzingatia masuala mahususi ya kimazingira ili kulinda nchi.

Pia, akijibu swali kuhusu udhibiti wa uchafuzi pembezoni mwa Ziwa Victoria ambao unapunguza samaki kuzaliana na shughuli za uvuvi kudorora, waziri huyo alisema Serikali imeandaa Kanuni na Miongozo kuhakikisha Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM), inafanyika kwa miradi ya maendeleo iliyopo na inayotarajiwa kufanyika pembezoni mwa ziwa hilo.

Aliongeza kuwa imeandaliwa mikakati pamoja na kuendelea kutekeleza katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki kwa ajili ya kubebea bidhaa ambayo kwa kiasi kikubwa ilikuwa ikichangia uchafuzi pembezoni mwa Ziwa hilo

Hata hivyo, Dkt. Jafo alibainisha kuwa uchafuzi wa mazingira unaofanyika pembezoni mwa ziwa unatokana na shughuli za kibinadamu zisizozingatia hifadhi ya mazingira zikiwemo utiririshaji wa majitaka kutoka katika maeneo ya makazi pamoja utupaji wa taka ngumu kutoka majumbani na viwandani.

Alitaja shughuli zingine kuwa ni kilimo kisicho endelevu kinachosababisha uchafuzi wa maji kutokana na kuongezeka kwa tabaki (segments) na matumizi yasiyo sahihi ya viuatilifu na mbolea za viwandani na uchimbaji wa madini usio endelevu.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted