Italia yatia saini mkataba wa gesi na Angola ikitaka kukomesha utegemezi kwa Urusi

Italia inataka kuongeza Angola na Congo-Brazzaville kwenye orodha ya mataifa wasambazaji wa gesi kuchukua nafasi ya Urusi, ambayo huisambazia Italia takriban asilimia 45 ya gesi

0

Italia siku ya Jumatano ilifanya mkataba na Angola ili kuongeza usambazaji wa gesi kutoka nchi hiyo ya kusini mwa Afrika huku ikihangaika kujiondoa kwa utegemezi wa gesi ya Urusi kutokana na vita vya Ukraine.

Makubaliano hayo yailitiwa saini kuendeleza ubia mpya wa gesi asilia na kuongeza mauzo ya nje kwa Italia, taarifa kutoka kwa waziri wa mambo ya nje wa Italia ilitangaza.

“Leo tumefikia makubaliano mengine muhimu na Angola ya kuongeza usambazaji wa gesi,”Waziri wa Mambo ya Nje Luigi Di Maio alisema katika taarifa hiyo.

“Ahadi ya Italia ya kupata vyanzo tofauti vya usambazaji wa nishati imethibitishwa,” Di Maio alisema mwishoni mwa ziara ya saa mbili na nusu mjini Luanda.

Waziri Mkuu Mario Draghi anataka kuongeza Angola na Congo-Brazzaville kwenye orodha ya mataifa ya wasambazaji kuchukua nafasi ya Urusi, ambayo huisambazia Italia takriban asilimia 45 ya gesi.

“Hatutaki kutegemea gesi ya Urusi tena, kwa sababu utegemezi wa kiuchumi haupaswi kutegemea mweleko wa kisiasa,” alisema katika mahojiano na gazeti laCorriere della Sera iliyochapishwa siku Jumapili.

“Ni muhimu kupata gesi kutoka mataifa mseto na tunatumai makubaliano haya yatatekelezwa kwa muda mfupi — haraka kuliko tulivyofikiria mwezi mmoja uliopita,”alisema.

Draghi alipaswa kuenda mwenyewe nchini Angola lakini baada ya kupimwa na kukutwa na Covid-19 alimtuma Di Maio na Waziri wa Mpito wa Ikolojia Roberto Cingolani.

Cingolani alielezea mpango huo kama “makubaliano muhimu ambayo yanatoa msukumo kwa ushirikiano kati ya Italia na Angola katika nyanja za nishati ya mimea, LNG na mafunzo ya teknolojia na mazingira.”

Mawaziri hao wawili, wakiandamana na Claudio Descalzi, mtendaji mkuu wa kampuni kubwa ya nishati ya Italia ENI, pia walikutana na Rais Joao Lourenco.

Baadaye walielekea katika nchi jirani ya Congo-Brazzaville ambako wanatarajiwa kukutana na Rais Denis Sassou Nguesso siku ya Alhamisi.

“Hizi ni harakati za kuhakikisha tunahifadhi gesi na mafuta kwa msimu ujao wa baridi,” alisema Francesco Galietti, mkuu wa shirika la ushauri la Policy Sonar lenye makao yake makuu Roma.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Angola Tete Antonio alielezea makubaliano hayo kama “muhimu sana.”

Tamko kama hilo litatiwa saini katika Jamhuri ya Congo.

Makubaliano hayo ya kupata vyanzo vya gesi kutoka mataifa hayo kunafuatia kufikiwa kwa makubaliano na Algeria na Misri katika wiki za hivi karibuni.

Algeria kwa sasa ni muuzaji mkuu wa pili kwa Italia, ikitoa karibu asilimia 30 ya matumizi yake.

ENI ilisema makubaliano na Sonatrach ya Algeria yatakuza usambazaji wa gesi kupitia bomba la chini ya bahari la Transmed kwa “hadi mita za ujazo bilioni tisa kwa mwaka” ifikapo 2023-24.

Transmed ilikuwa na bomba la ziada la mita za ujazo bilioni 7.8 kwa mwaka mnamo 2021 — ingawa imesema iko tayari kuongezai mabomba.

Italia pia imekuwa katika mazungumzo na Azerbaijan kuhusu upanuzi wa Bomba la Trans-Adriatic (TAP).

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted