UN: Watoto ni kati ya watu 13 waliouawa katika machafuko ya DR Congo wiki hii

Mapigano yameongezeka katika miezi ya hivi karibuni baada ya waasi wa M23 kuishutumu serikali kwa kushindwa kuheshimu makubaliano ya mwaka 2009 ambapo jeshi lilipaswa kuwajumuisha wapiganaji hao kwenye...

0
waandamanaji wakiwa wamebeba bango la kuunga mkono wanajeshi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wakati wa maandamano huko Goma mnamo Juni 15, 2022 – . (Photo by Aubin Mukoni / AFP)

Takriban raia 13, wakiwemo watoto wanne, waliuawa katika mapigano mapya mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wiki hii, Umoja wa Mataifa ulisema, huku kukiwa na ongezeko la mapigano kati ya jeshi na waasi.

Mapigano yameongezeka katika miezi ya hivi karibuni baada ya waasi wa M23 kuishutumu serikali kwa kushindwa kuheshimu makubaliano ya mwaka 2009 ambapo jeshi lilipaswa kuwajumuisha wapiganaji hao kwenye jeshi.

Ghasia zilizozuka upya tayari zimewalazimu maelfu kukimbia makazi yao mashariki mwa DRC, na kuweka shinikizo kwa mashirika ya kibinadamu katika eneo hilo.

Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu (OCHA) ilisema Jumatano kwamba raia 13 walikufa katika mapigano kati ya Juni 19 na Juni 21 katika eneo la Rutshuru huko Kivu Kaskazini.

Makumi ya maelfu wamelazimika kukimbia.

“Vijiji kadhaa katika eneo la Rutshuru vimekosa wakazi wake, baadhi yao wakikimbilia Uganda,”OCHA ilisema.

Watu wanakimbilia nchi jirani ya Uganda, au katika maeneo salama mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ambako “kwa sasa wanahifadhiwa katika shule, viwanja vya michezo na maeneo mengine ya pamoja,” iliongeza.

Takriban watu 158,000 wamelazimika kutoka makwao tangu mwezi Machi huko Rutshuru na Nyiragongo kutokana na mapigano kati ya jeshi la Congo na M23, Umoja wa Mataifa ulisema.

OCHA ilisema hitaji linaloongezeka la usaidizi wa kibinadamu “linazuiwa na kuendelea kwa ghasia.”

Baada ya kukaa kimya kwa miaka mingi, waasi hao walianza tena mapigano Novemba mwaka jana.

Wanamgambo wa Kitutsi wa Congo ambao ni miongoni mwa makundi mengi yenye silaha mashariki mwa DRC, M23 walijinyakulia umaarufu duniani mwaka 2012 walipouteka mji mkuu wa Kivu Kaskazini Goma.

Ililazimishwa kuondoka muda mfupi baadaye katika mashambulizi ya pamoja ya wanajeshi wa Umoja wa Mataifa na jeshi la Congo.

Lakini wanamgambo hivi karibuni wamerejea tena, wakipambana mara kwa mara na wanajeshi wa Congo katika ghasia ambazo zimezusha mvutano katika Afrika ya Kati.

Mashambulizi mapya yamefufua chuki za miongo kadhaa kati ya Kinshasa na Kigali, huku DRC ikiilaumu nchi jirani ya Rwanda kwa kuzuka upya kwa wanamgambo hao. Rwanda imekanusha mara kwa mara kuwaunga mkono waasi, huku nchi zote mbili zikilaumiana kwa kufanya mashambulizi ya kuvuka mpaka.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted