UN: Takriban watu 471 wamekufa, kujeruhiwa au kutoweka katika ghasia za magenge Haiti

Magenge ambayo yamekuwa yakiendeleza mauaji bila kuadhibiwa kwa kiasi kikubwa yameweza kufikia vitongoji duni vya mji mkuu wa Haiti, wakitekeleza wimbi la utekaji nyara.

0

Takriban watu 471 waliuawa, kujeruhiwa au kutoweka kutokana na mapigano makali mwezi huu kati ya magenge hasimu katika mji mkuu wa Haiti Port-au-Prince, Umoja wa Mataifa ulisema Jumatatu.

“Matukio makubwa ya unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na wasichana pamoja na wavulana waliojumuishwa kwenye makundi ya magenge pia yameripotiwa,” Umoja wa Mataifa ulisema katika taarifa kuhusu idadi ya watu waliofariki kutokana na ghasia kati ya Julai 8 na 17 katika kitongoji masikini cha Cite Soleil.

Haikubainisha ni wangapi kati ya watu hao waliuawa.

Takriban watu 3,000 wamekimbia makazi yao, miongoni mwao mamia ya watoto wasio, na takriban nyumba 140 zimeharibiwa, ilisema taarifa hiyo.

“Mahitaji ya kibinadamu katika eneo la Cite Soleil ni makubwa na yanaongezeka kutokana na umaskini, ukosefu wa huduma za msingi, ikiwa ni pamoja na usalama, na kuongezeka kwa ghasia za hivi karibuni,” Ulrika Richardson, mratibu wa misaada ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Haiti, alisema katika taarifa hiyo.

Wakati mashirika ya Umoja wa Mataifa yanatoa msaada katika Cite Soleil, “mbinu endelevu zaidi na ya kiujumla inahitaji kupatikana kwa ajili ya maendeleo ya muda wa sasa na wa baadae  ili kukabiliana na matatizo ya kila mara,” Richardson aliongeza.

Magenge ambayo yamekuwa yakiendeleza mauaji bila kuadhibiwa kwa kiasi kikubwa yameweza kufikia vitongoji duni vya mji mkuu wa Haiti, wakitekeleza wimbi la utekaji nyara.

Angalau visa 155 vya utekaji nyara 155 vilifanyika katika mwezi wa Juni, ikilinganishwa na 118 mwezi Mei, kulingana na ripoti iliyotolewa na Kituo cha Uchambuzi na Utafiti wa Haki za Binadamu.

Waziri Mkuu Ariel Henry bado hajatoa maoni yake kuhusu kuzuka kwa ghasia zilizokumba Cite Soleil mapema Julai.

Haiti imezama katika mzozo wa kisiasa uliotokana na uchaguzi wa 2016, ambao ulichochewa na mauaji ya rais Jovenel Moise nyumbani kwake mnamo Julai 7, 2021.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted