Shahidi wa nne katika kesi ya Kikatiba ambaye ni Mkuu wa Gereza la Ukonga Edward Shabani amesema hafahamu wala hajui kwamba Tundu Lissu ni Wakili kitaaluma na aliwahi pia kuwa Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika(TLS).

Ameyasema hayo leo Julai 23,2026 kwenye ushahidi wake wakati akiulizwa maswali ya dodoso na Wakili wa waleta maombi kutoka TLS ambao kimsingi wanamaslahi na shauri hilo, Wakili Emmanuel Ukashu muda mfupi kabla ya kusawazisha maswali ya dodoso kutoka jopo la mawakili wa Jamhuri.
Katika hoja hizo Wakili Ukashu pia alimuuliza shahidi iwapo anajua chochote kuhusu maelekezo kutoka ambapo shahidi alijibu kwa uelewa wake ni maelekezo ya kiutendaji.
Wakili: Nitakua sahihi kusema kwamba waleta maombi wote ni mawakili.
Shahidi: Sahihi
Wakili: Nitakua sahihi nikisema mleta maombi namba 4 ambaye ni mshtakiwa Lissu ni Wakili.
Shahidi: Sifahamu.
Wakili: Nitakua sahihi nikisema mleta maombi 4 aliwahi kuwa Rais wa TLS.
Shahidi: Sifahamu
Wakili: Kwa kiapo chako ulicholeta hapa Mahakamani ili mtu aweze kuingia Gerezani maana yake taarifa zake zimehakikiwa na wewe.
Shahidi: Sahihi
Wakili: Nitakua sahihi bosi wako ni Kamishina General wa Magereza
Shahidi: Sahihi
Wakili: Kwa uelewa wako ukiambiwa malekezo kutoka juu Unaelewa nini.
Shahidi: Ni maelekezo ya kiutendaji
Wakili: Usipoyafanya haufukuzwi kazi
Shahidi: Inategemea
Wakili: Unajua taaluma ya Sheria inaheshimiwa sana
Shahidi: Najua
Wakili: Unajua kwamba Wakili anatakiwa awe na chumba chake
maalum kwa ajili ya kuongea na mteja wake.
Shahidi: Najua.
Wakili Ukashu alihitimisha hoja hiyo akimpa kijiti Wakili Edson Kilatu ambaye katika msingi wa hoja zake kwa Shahidi alimuuliza shahidi juu ya utaratibu wa watu kuingia gerezani kwenye kuona ndugu au kama ni wakili kwenda kuonana na wateja wake.
Wakili: Ni sahihi kuna kitabu ambacho raia wa kawaida wakiingia ni lazima wawe wanasaini
Shahidi:Sahihi
Wakili: Na ni sahihi vile kuna kitabu cha Mawakili kusaini
Shahidi: Ni sahihi
Wakili: Na ni sahihi vilevile kuna watu wanaosimamia wanaoingia
Shahidi: Ni sahihi
Wakili: Ni sahihi kwamba vitabu vya pale kwenye geti la kuingia wanasaini
Shahidi: Ni sahihi
Wakili: Ni sahihi kwamba kwa utaratibu inatakiwa kujiandikisha na kwa waliokataliwa kuingia kumuona ndugu au kama wakili kumuona mteja wake ni lazima iandikwe kwanini alikataliwa.
Shahidi: Sina Uhakika
Wakili: Ilizungumziwa suala la ukaguzi wa nyaraka hapa, sasa umeleta kiapo cha afisa yoyote ambaye alikagua hizo nyaraka
Shahidi: Sijaleta
Wakili: Ni sahihi kwamba bwana Lecha ambaye ni Msaidizi wako hajaleta kiapo chochote.
Shahidi: Anayetakiwa kuleta hicho kiapo ni Mkuu wa Gereza kwa ajili ya watendaji wote.
Wakili: Wakati unahojiwa na Lissu ulizungumzia kwamba ya kitu ambacho umekubali ni kwamba Lissu ameleta orodha ya watu ambao amewaleta
Shahidi: Ni sahihi
Wakili: Na ni sahihi kwamba wewe unakua unaruhusu watu ambao hawajawekwa kwenye Orodha kuonana na Lissu
Shahidi: Inategemea
Katika maswali ya kusawazisha yaliyoulizwa na Wakili wa Serikali Francis Wisdom, Shahidi aliieleza Mahakama kwamba, suala la mtu kuandikisha au kufanyiwa ukaguzi ni la lazima na kuhusu mshtakiwa kulindwa analindwa wakati wote mpaka kesi itakapoisha.
Shauri hili la kikatiba namba 7300/2026 leo limehitimishwa baada ya mashahidi kumaliza kutoa ushahidi kwa siku nne mfululizo, na sasa kinachosubiriwa ni uamuzi ambapo Mahakama chini jopo la majaji watatu wakiongozwa jaji Amiri Mruma, wamepanga tarehe 16 Septemba 2026, kuja kwa ajili ya kutaja tarehe ya uamuzi
Katika shauri hilo, mawakili Kulwa Maduhu, Nashon Nkung na Paul Kisabo wanailalamikia Mamlaka ya Magereza kwa madai ya kuwazuia kuingia Gereza la Ukonga kumwona mteja wao na kutowapatia faragha ya kufanya mazungumzo naye waliporuhusiwa kuingia gerezani.