Jina la Rais Mwinyi laibuka kwenye kesi ya Mbowe

Jina hilo limeibuliwa na wakili wa utetezi John Mallya wakati akimuhoji shahidi maswali

0
Rais Hussein Mwinyi wa Zanzibar

Shahidi wa tisa katika kesi inayomkabili mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe na wenzake watatu ameiambia Mahakama jana Alhamisi kuwa, namba 0784 779944 ambayo imesajiliwa kwa jina la Freeman Aikael Mbowe ambaye ni mwenyekiti wa CHADEMA  ilifanya muamala wa kutuma pesa kiasi cha shilingi 80,000 kwenda namba 0782 237913 yenye jina la usajili Halfan Bwire Hassan ambaye ni mshatakiwa wa kwanza katika kesi hiyo ya Ugaidi

Shahidi huyo Gladys Fimbari (39), Mwanasheria wa kampuni ya Airtel Tanzania, ameanza kutoa ushahidi huo jana mbele ya Jaji Joachim Tiganga, akiongozwa na wakili mwandamizi wa Serikali Jenitreza Kitale, ambapo amesema kuwa mwaka 2014 mwezi wa nane, aliajiriwa kama ofisa sheria, lakni Machi, 2021 alibadilishwa cheo na kuwa meneja kitengo cha sheria.

Amesema ipo mifumo ya taarifa inayolinda taarifa hizo lakini kitengo chake anaruhusiwa kutoa taarifa za watu kwenye taasisi iwapo zinahitajika kwa ajili ya uchunguzi.

Taarifa ninazotoa za kiuchunguzi kwa taasisi au vyombo vya kiuchunguzi ni Jeshi la Polisi, PCCB, Tume ya kuzuia na kupambana na dawa za kulevya, TCRA na tunatoa kwa FIU (Financial Intelligence Unit) na mteja binafsi pia anaruhusiwa kupewa taarifa.

Vyombo hivyo huwa vinaomba taarifa za miamala ya kifedha, kupiga na kupokea simu pamoja na usajili” – amesema shahidi huyo.

Akiendelea kutoa ushahidi huo Glady ametaja tarehe tofauti zilizoonyesha namna ambavyo miamala ya fedha ilivyokuwa ikifanyika ikimuhisha Freeman Mbowe, Halfani Bwire na Denis Urio

Haya ni baadhi ya mahojiano yalivyokuwa kati ya wakili mwandamizi wa Serikali Jenitreza Kitale na Shahidi

Wakili wa Serikali: Unafanya kazi wapi: 

Shahidi: Nafanya kazi Airtel Tanzania 

Wakili wa Serikali: Unafanya Kazi kama nani 

Shahidi: Awali niliajiriwa Kama Afisa wa Sheria. Baadae 2021 Mwezi March nilibadilishwa Cheo na Kuwa Meneja Kitengo cha Sheria 

Wakili wa Serikali: Ifahamishe Mahakama kampuni ya AIRTEL PLC inajihusisha na nini

Shahidi: Inajihusisha na Kupiga na Kupigiwa Simu, Huduma ya Miamala ya Fedha kupitia Airtel Money

Wakili wa Serikali: Sasa hiyo Kampuni ya AIRTEL PLC Inatoa hizo huduma kaa Watu gani 

Shahidi: Ili Upate huduma kutoka Airtel lazima uwe na simu handset na lazima uwe na Simcard ya Airtel 

Baada ya hapo mtu anayemhudumia atachukua majina yake na kumuunga katika mifumo yetu na kisha mteja atatakiwa aweke dole gumba na msajili wetu atafanya uhakiki kupitia mifumo ya Nida amabayo imeunganishwa na mifumo yetu ya usajili.

Baada ya kufanya uhakiki, atakapopata taarifa kutoka Nida kuhusiana na uhakiki wa namba.

Baada ya kupata uhakikiki, Nida watatoa taarifa za mteja na taarifa zote zitahifadhiwa kwenye mfumo iliyounganishwa na hapo usajili utakuwa umekamilika.

Shahidi: Mteja anapotoa majina yake pamoja na namba ya Kitambulisho Cha Nida, zile taarifa zinahakikiwa na Ofisa wetu Airtel kwa ajili ya kuhakikia na kwamba mifumo yetu imeunganishwa na Nida.

Wakili wa Serikali: Ifafanulie Mahakama Vizuri, umesema Afisa Usajili Wa Airtel atafanya Uhakiki kutoka NIDA, Je Afisa wenu usajili anapataje taarifa kutoka NIDA?

Shahidi:Ofisa Msajili wa Airtel anapata taarifa kutoka Nida kutokana na mifumo yetu imeunganishwa na Nida.

Wakili wa Serikali: Sasa ieleze Mahakama Juu ya Mfumo wa MOBIQUIT Jinsi unavyofanya kazi katika Utunzaji Wa Kumbukumbu za Miamala

Shahidi: Mfumo wa business Intelligence ni pale ambapo mteja anapofanya mawasiliano akiwa karibu na mnara, yale mawasiliano yake yanachukuliwa na kwenda kutunzwa kwenye server na baada ya hapo unapotaka kuifikia hii taarifa unatumia mfumo huu wa business Intelligence.

Mawasiliano haya ni pale mtaja anapopiga simu, anapopokea simu na hata anapotumia huduma ya internet.

Mifumo hiyo miliwi niliyoitaja nimeitumua tangu nilipojiunga na Airtel mpka sasa, lakini mwaka 2019 ndio nilianza kutumia mfuno wa Agile.

Shahidi: Taarifa ninazotoa za kiuchunguzi kwa taasisi au vyombo vya kiuchunguzi ni Jeshi la Polisi, PCCB, Tume ya kuzuia na kupambana na dawa za kulevya, TCRA na tunatoa kwa FIU (Financial Intelligence Unit) na mteja binafsi pia anaruhusiwa kupewa taarifa.

Vyombo hivyo huwa vinaomba taarifa za miamala ya kifedha, kupiga na kupokea simu pamoja na usajili.

Shahidi: Taratibu za kuomba taarifa za kuchunguzi ni hizi hapa,

Kwanza, chombo au taasisi ya kuomba uchunguzi huwa ina leta barua ya maombi na maombi haya yanawasilishwa katika kampuni ya Airtel kupitia upande wetu wa mapokezi, yakishapokelewa yananakiliwa katika kitabu chetu na kupelekwa kitengo cha sheria na baada ya hapo Mkuu wetu wa Kitengo cha sheria anasaini kuyafanyia kazi maombi hayo.

Baada ya kukamilisha vitu vyote, ofisa Sheria ana hakiki barua hiyo na kiuchunguza vizur ikiwemo anuani husika na nembo husika na kuhakiki ni taarifa gani zimeombwa? Na je taarifa hizo Ni za kiuchunguzi? Na kama taarifa hizi sio za kiuchunguzi hatuwezi kuzifanyia kazi, pia barua hiyo iwe na mhuri kutoka taasisi husika.

Watu wanaoshughulikia maombi haya ya kiuchunguzi ni wawili ambao ni mimi na mwenzangu.

Shahidi: Baada ya kujiridhisha tunaingia katika mifumo niliyoitaja hapo awali.

Ninapoingia katika kompyuta yangu nainginza Username na Password.

Username na Password naipata kutoka Kitengo cha IT ambapo mimi peke yangu ndio nafahamu na baada ya hapo naingia katika mfumo.

Baada ya hapo naingiza namba ya simu ya mteja na muda ninaoangalia hizo taarifa.

Baada ya kuingia katika mfumo huo, nachakata taarifa na kutozitoa huko zilipohifadhiwa na kuzileta kwenye page yangu.

Wakili: Hebu tueleza kipindi network inapokuwa down taarifa mlizotunza kwenye server huwa zinakuwaje?

Shahidi: Network inapokuwa down, haiwezi kuathiri mifumo yetu au taarifa zilizopo ndani ya mifumo huwa haziguswi au kupata changamoto

Wakili Kitale: Umesema hapa mifumo yenu ni Intelligent (uadilifu) hebu ieleze mahakama uadilifu wa mifumo yenu ikoje?

Shahidi: Hakuna mtu wa kuingilia mifumo, unafanya kazi vizuri muda wote na tuna software ambayo tumeweka ili kuangalia usalama wetu.

Wakili Kitale: Mnamifumo ipi?

Shahidi: Tuna mifumo mitatu.

Mfumo wa kwanza unaitwa Mouituity, hiyo ni kuchukua taarifa za mteja na kuhifadhiwa katika server na endapo tunahitaji kupata taarifa za miamala tunaweze kuangalia katika mfumo huu.

Mfumo wa pili ni Agile- ambapo inahusika na usajili na uhakiki wa namba ya mteja.

Mfumo wa watatu ni Business Intelligence.

Wakili Kitale: Unakumbuka Nini mnamo tarehe 2 mwezi wa saba mwaka 2021?

Shahidi: Julai 2, 2021 nilikuwa ofisi za Airtel Morocco nikiwa nafanya majukumu yangu.Siku hiyo nikiwa ofisini alikuja Mkuu wa Idara ya Sheria wa Airtel, alinielekeza mimi nishughulikie maombi kutoka ofisi ya uchunguzi wa kisayansi ya Jeshi la Polisi.

Maombi hayo yalikuwa yanataka taarifa za miamala ya fedha katika namba 0782 237913 na namba nyingine ilikuwa 0787 555200 na namba ya tatu ilikuwa 0784 779944 pia barua hiyo iliomba niangalie taarifa za usajili za line hizo.

Baada ya hapo, nilihakiki ile barua address yake kama inatoka taasisi husika, niliangalia barua hiyo kama kweli inaaongelea uchunguzi, taarifa zinazoombwa ni za muda gani na kuhakikisha kama kweli line hizo zimesajiliwa.

Baada ya kujiridhisha niliingia katika kituo changu cha kompyuta kisha nikaingia katika mfumo wa Agile na nikaingiza namba moja ya simu ambayo imeombewa taarifa na kisha ikanitolea taarifa inayohusiana.

Shahidi: Nilipata taarifa za usajili wa namba 0787555200, 0782237913 na 0784 779944 na kisha nikaprint nyaraka zote tatu baada ya kupata taarifa.

Katika mfumo wa obiquity ni lazima uingize namba na muda hivyo nilifanya hivyo kwa namba za simu zote tatu.

Barua hiyo ya Polisi iliomba taarifa za line zote tatu kuanzia 1/6/2020 mpaka 31/7/2020.

Baada ya taarifa hizo kuonekana katika mfumo, nilijiridhisha na kuprint taarifa zote.

Baada ya kuprint, nyaraka hizo nilweka mhuri na kuweka sahihi pamoja na tarehe husika.

Pia niliandaa barua kwa ajili ya kuambatanisha taarifa ambazo niliandaa.

Wakili Kitale: Ukiona barua hizo utazitambuaje?

Shahidi: Nitazitambua kwa saini yangu, mhuri wa kampuni ya Airtel PLC, tarehe husika na namba za simu ambazo nimezitolea taarifa ambazo ni 0787 555,200, 0782 237913 na 0784779944.

Kuhusu taarifa za miamala ya fedha ambayo nimeitolea taarifa katika simu hizo, Nitazitambua kwanza namba za simu ambazo zinaonekana katika ile taarifa, mhuri wa kampuni, saini yangu na tarehe.

Wakili Kitale: Shahidi hebu shika nyaraka hizi na utuonyeshe ipi ni taarifa ya miamala ya fedha ipi ni taarifa ya usajili wa namba hizo.

Shahidi amezitambua nyaraka hizi moja baada ya nyingine kwa kuzionyesha mahakaman.

Shahidi: Naomba mahakama ipokee nyaraka hizi zitumike kielelezo katika kesi hii

Upande wa mashtaka wamewapatia nyaraka hizo mawakili wa upande wa uetetezi ili waweze kuzipitia.

Kibatala: Mheshimiwa jaji kwani niaba ya mshtakiwa wa nne (Freeman Mbowe) hatuna pingamizi dhidi ya nyaraka hizi.

Wakili Mtobesya: Kwa niamba ya mshtakiwa wa kwanza (Halfan Bwire)  Hatuna pingamizi.

Wakili Mallya: Kwaniaba ya mshtakiwa wa pili (Adam Kasekwa) hatuna pingamizi.

Wakili Matata: Mheshimiwa Jaji kwa niaba ya mshtakiwa wa tatu (Mohamed Ling’wenya) hatuna pingamizi.

Shahidi: Katika namba 0784 779944 imesajili kwa jina la Freeman Aikaeli Mbowe (Mshtakiwa wa nne) katika kesi hiyo.

Shahidi: Namba 0787 555 200 imesajiliwa kwa jina la Denis Leo Urio.

Shahidi: Namba ya simu 0782 237913, imesajiliwa kwa jina la Halfan Bwire Hassan (Mshtakiwa wa kwanza katika kesi hiyo)

Shahidi:  Muamala iliyotumwa tarehe 20/7/2020 kwenye namba 0787 555 200, ambayo kwa mujibu wa kielelezo namba 20, namba hiyo imesajiliwa kwa jina la Denis Leo Urio, ilipokea Sh 500,000 kutoka kwenye namba ambayo ni Collection Account 780900174, na mhusika mwenye namba ya Airtel 0787 555200 alikuwa na salio kiasi cha Sh 46, 646 katika simu yake na hivyo akawa na jumla ya kiasi cha Sh 546,646 baada ya kuingizwa Muamala wa Sh 500,000

Shahidi: Pia tarehe 22/7/2020, namba ya simu ya Denis Urio (0787 555 200) ilipokea fedha Sh 199,000 kutoka namba 0780 900244.

Shahidi: Tarehe 31/7/2020 namba 0784 779944, ambayo katika kielelezo namba 21,  imesajiliwa kwa jina la Freeman Aikaeli Mbowe, ilituma fedha kiasi cha Sh80,000 kwenda namba 0782 237913 yenye jina la usajili Halfan Bwire Hassan.

Shahidi: Hiyo Tarehe 20/7/2020 Muamala mwingine uliofanyika kwa namba ya 0787 555200 alituma kiais Cha Sh 300,000 kwenda namba 0785191954.

Wakili Kitale: Mheshimiwa Jaji kwa upande wetu ni hayo tu.

Mahojiano hayo yaliyochukua zaidi ya saa moja kati ya Jamhuri na Shahidi yalitoa nafasi kwa upande wa utetezi nao kumuuliza shahidi ambapo mambo mengi yaliibuka katika mahojiano yao ikiwamo uhalali wa namba zilizotajwa lakini pia jina la aliyekuwa Waziri wa Ulinzi wakati huo ambaye kwa sasa ni Rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Mwinyi.

Jina hilo liliibuliwa na Wakili wa utetezi John Mallya wakati akiendelea kumuuliza shahidi maswali jambo ambalo limemfanya Jaji Tiganga kumuuliza Mallya ni wapi ametoa maelezo hayo.

Haya ni baadhi ya mahojiano ya Wakili wa utetezio John Mallya na Shahidi.

Mallya: Kwenye hiyo Barua Uliombwa Transactions Za Watu Wangapi?

Shahidi: Haija’ specify 

Mallya: Tunakubaliana kuwa Umeombwa Miamala ya Namba Ngapi 

Shahidi: Tatu 

Mallya: We umepeleka mingapi 

Shahidi: Miwili 

Mallya: Kwa nini? 

Shahidi: Oversight, (Kupitiwa tu)

Mallya: Mimi siamini kuwa ulipitiwa.. 

Mallya: Hebu nisomee muamala wa mwisho kwenye Kielelezo namba 20 una Involve TSh 80,000? 

Shahidi: Ndiyo elfu 80,000 

Mallya: Namba hiyo uliombwa kutoa miamala yake? 

Shahidi: Ndiyo

Mallya: Kwenye Miaamala ya Khalfani Bwire unasema Kuna Kupitiwa, Je sisi tutajua Kuna Kupitiwa Mara Ngapi? 

Shahidi: Hatuwezi kujua

Mallya: Unafahamu makosa wanayoshitakiwa hawa watuhumiwa wanne? 

Shahidi: Hapana 

Mallya: Basi mimi nakufahamisha kuwa mshtakiwa wa nne, Bw. Freeman Mbowe Anashitakiwa kwa kuwatumia hawa pesa ya kufanyia Ugaidi…

Mallya: Nikisema unaleta makusudi muamala wa Khalfani Bwire ambao umeombwa, Ila Kwa sababu Khalfani Bwire alikuwa anafanya Ugaidi Na Kingai Ukaona usilete Mahakamani??? 

Shahidi: Mh. Jaji bado nasimamia jibu langu kuwa nilipitiwa.

Mallya:Sasa kwenye miamala ya Khalfani Bwire, inaonyesha alikuwa anatumiwa fedha na Waziri wa Ulinzi kipindi kile ambaye ni Hussein Mwinyi ambaye sasa ni Rais wa Zanzibar, Ila wewe ukaona ufiche tusione miamala hiyo.. 

Jaji: Bwana Mallya, Unatoa wapi maelezo hayo?

Mallya: Kwa mteja wetu mheshimiwa Jaji 

Jaji: Ilikuwa chini ya kiapo? 

Mallya: Hapana, lakini wateja wetu wanatupatia taarifa za kesi yao kila siku 

Jaji: Nafikiri si vyema kutaja watu wasiokuwepo Mahakamani, au mna mpango wa kumuita Rais Hussein Mwinyi Mahakamani?

Mallya: Ndiyo mheshimiwa Jaji tutamuita tukihitaji baada ya kupata miamala ya bwire 

Jaji: Basi naomba watu ambao hawapo Mahakamani na hajawajitokeza kwenye proceedings tusiwataje sababu wanaweza wasipate nafasi ya kuja Mahakamani kujitetea 

Mallya: Sawa Mheshimiwa Jaji

Mallya: Shahidi makosa yako ya kutokuleta miamala ya Bwire, Je nani atakuja Kurekebisha Kosa hilo? 

Shahidi: Sifahamu 

Mallya: Je taarifa zenu za usajili (Format) zina fanana? 

Shahidi: Ndiyo muundo au format unafanana

Mallya: Kwenye Kielelezo namba 20 miamala wa tarehe 20 July 2020, ulisema P to P maana yake ni nini 

Shahidi: Airtel kwenda Airtel 

Mallya: na hiyo Cash in..? 

Shahidi: Namba ya mhusika ambayo imepokea 

Mallya: Ikipokea Kutoka kwa wakala itaandikaje?

Mallya: katika hawa Washtakiwa wanne kuna hata mmoja kasajiliwa kama Wakala?

Shahidi: Miye sifahamu.. 

Mallya: Mheshimiwa Jaji nina maswali bado kwa Shahidi wetu, na muda umetutupa mkono, ningeleta ombi kwako tuhairishe hadi kesho(leo) tuendelee na Mahakama.

Kuibuliwa kwa jina la Rais wa Zanzibar Hussein Mwinyi imezua mjadala mkubwa katika mitandao ya jamii, ambapo baadhi ya wanachama na mashabiki wa chama kikuu cha upinzani CHADEMA wametaka kesi hiyo ifutwe au Rais Hussein Mwinyi aunganishwe kwenye kesi hiyo

Jaji Joachim Tiganga aliahirisha kesi hiyo hadi January 14, ambapo shahidi ataendelea kutoa ushahidi wake akihojiwa na mawakili wa utetezi.

Mbowe na wenzake wanakabiliwa na mashtaka sita, yakiwamo ya kufadhili vitendo vya ugaidi, kukutwa na silaha aina ya bastola pamoja na sare za jeshi kinyume cha sheria.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted