Mwanajeshi aliyeongoza mapinduzi Burkina Faso aapishwa kuwa rais

Paul-Henri Sandaogo Damiba alitawazwa kuwa rais siku ya Jumatano, zaidi ya wiki tatu tu baada ya kuongoza mapinduzi ya kumuondoa madarakani Rais Roch Marc Christian Kabore.

0
Rais wa Burkina Faso Paul-Henri Sandaogo Damiba

Mwanajeshi aliyeongoza mapinduzi Burkina Faso Luteni-Kanali Paul-Henri Sandaogo Damiba alitawazwa kuwa rais siku ya Jumatano, zaidi ya wiki tatu tu baada ya kuongoza mapinduzi ya kumuondoa madarakani Rais Roch Marc Christian Kabore.

Katika hafla iliyoonyeshwa kwenye televisheni, Damiba aliapa mbele ya waburkinabe “kuhifadhi, kuheshimu, kudumisha na kutetea Katiba.”

Damiba alikuwa amevalia sare za jeshi na bereti nyekundu, na alivaa mkanda wenye rangi za bendera ya taifa la Burkina Faso.

Vyombo vya habari vya humo nchini pekee ndivyo vilivyoruhusiwa kuhudhuria hafla hiyo katika chumba kidogo katika ofisi za Baraza la Katiba.

Mnamo Januari 24, Damiba, 41, aliongoza wanajeshi wengine kumuondoa uongozini Kabore kufuatia hasira ya umma juu ya jinsi alivyoshughulikia uasi wa kijihadi wa umwagaji damu.

Wiki iliyopita, Baraza la Katiba liliamua rasmi kwamba Damiba alikuwa rais, mkuu wa nchi na kamanda mkuu wa majeshi.

Hatua hiyo ilithibitisha tangazo la jeshi mnamo Januari 31 kwamba Damiba atateuliwa katika majukumu hayo kwa kipindi cha mpito, na kusaidiwa na makamu wawili wa rais.

Burkina Faso ni mojawapo ya nchi maskini zaidi duniani na mojawapo ya nchi ambazo zimepitia hali tete barani Afrika.

Nchi hiyo imekumbwa na mapinduzi ya mara kwa mara tangu lipate uhuru kutoka kwa Ufaransa mwaka 1960. Tangu mashambulizi ya kwanza ya wanajihadi mwaka 2015, zaidi ya watu 2,000 wamefariki, kwa mujibu wa takwimu za AFP, huku shirika la dharura la nchi hiyo likisema zaidi ya watu milioni 1.5 wamekimbia makazi yao.

– Kumhusu Damiba

Damiba amekuwa na uzoefu wa moja kwa moja na uasi.

Kabla ya kunyakua mamlaka, alikuwa kamanda wa Mkoa wa 3 wa Kijeshi, eneo lilioko katika mashariki mwa Burkina Faso — mojawapo ya maeneo yaliyoathirika zaidi na umwagaji wad amu.

Chanzo cha kijeshi baada ya kunyakua mamlaka kilisema kuwa “kamanda huyo amekuwa mstari wa mbele na wanajeshi waki.”

Kabla ya mapinduzi hayo, Damiba alikosoa mikakati iliyokuwepo ya kupambana na wanajihadi, akichapisha kitabu Juni mwaka jana kiitwacho “West African Armies and Terrorism: Uncertain Answers?”

Serikali ya kijeshi ilisimamisha katiba mara moja baada ya kuchukua mamlaka mnamo Januari 24, lakini baadaye ilibatilisha hii kutokana na shinikizo kutoka kwa majirani wa Afrika Magharibi wakitaka kurejeshwa kwa utawala wa kiraia.

Mamlaka za kijeshi zimeahidi kurejesha “uongozi wa kikatiba” ndani ya “wakati unaofaa” lakini suala la tarehe ya uchaguzi bado halijatatuliwa.

Mnamo Februari 5, jeshi ilitangaza kwamba tume ya wanachama 15 itakuwa na jukumu la “kutayarisha rasimu ya katiba na ajenda, pamoja na pendekezo la muda wa kipindi cha mpito.”

Burkina Faso imesimamishwa uanachama wa Jumuiya ya Afrika Magharibi ECOWAS, ingawa hadi sasa imeepuka vikwazo zaidi, tofauti na Guinea na Mali.

Pia imesimamishwa na ECOWAS, Jumuiya ya Kiuchumi ya mataifa 15 ya Afrika Magharibi.

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa mnamo Februari 9 lilionyesha “wasiwasi mkubwa” juu ya “mabadiliko ya serikali kinyume na katiba, “lakini lilichagua kutoyaelezea kama mapinduzi ya kijeshi au hata kuyashutumu moja kwa moja.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted