Hospitali Muhimbili yakana kuhusika na kusambaza video za Prof Jay akiwa ICU

Video hiyo iliyosambazwa mitandaoni inamuonesha msanii huyo akiwa chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum yaani ICU.

0
Joseph Haule(Prof.Jay), msanii wa HIP POP Tanzania

Hospitali ya Taifa Muhimbili imesema inashirikiana na mamlaka nyingine kumpata mtu aliyemrekodi video msanii wa Hip pop nchini Tanzania Joseph Haule maarufu kama Prof. Jay, ambaye anapatiwa matibabu hospitalini hapo. 

Video hiyo iliyosambazwa mitandaoni inamuonesha msanii huyo akiwa chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum yaani ICU.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na uongozi wa hospitali ya Muhimbili, imeeleza kusikitishwa na kitendi hicho na kulaani vikali kwani kitendo hicho ni kinyume na sheria.

Hospitali ya Taifa Muhimbili imesema kuwa haihusiki katika kurekodi na kusambaza video hiyo kama ambavyo inasemwa na watu kupitia mitandao ya kijamii.

Aidha kwa sasa inafuatilia kwa ukaribu tukio hilo ili kubaini chanzo cha video hiyo ili hatua stahiki zichukuliwe kwa muhusika au wahusika.

“Hiki ni kiwango cha juu cha kukosa utu na maadili.Tunatoa pole kwa mke wa Prof.Jay, familia na jamii nzima iliyoguswa na tukio hili” imesema taarifa hiyo.

“Tunahudumia wagonjwa takribani 3,400 kwa siku wakiwemo wananchi wa kawaida, viongozi wakuu wa Serikali, wanasiasa na watu wengine kwa kuzingatia taaluma maadili, utu na faragha” 

Hata hivyo hospitali hiyo imewaomba wananchi kuwa na imani nayo ikiwa ni pamoja na kuheshimu taratibu za Hospitali zilizowekwa.

Prof Jay mbali na kuwa msanii amewahi kuwa mbunge wa jimbo la Mikumi nchini Tanzania kupitia chama cha CHADEMA na pia ni mjumbe wa kamati kuu ya chama hicho.

Amelazwa katika hospitali hiyo yapata zaidi ya mwezi mmoja sasa akiwa chini ya uangalizi maalum, ingawa bado familia haijaweka wazi ugonjwa unaomsumbua.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted