Tanzania yelegeza Masharti ya wasafiri wanaoingia nchini humo.

Hii ni baada ya wimbi la Maambukizi ya virusi vya corona kupungua duniani kote

0
Waziri wa Afya nchini Tanzania, Ummy Mwalimu.

Serikali ya Tanzania imelegeza masharti ya wasafiri wanaoingia nchini kuanzia leo Machi 17,2022, ambapo kunaondolewa hitaji la kuwa na cheti cha kipimo(Negative RT-PCR Certificate), kilichokuwa kikihitajika hapo awali.

Hatua hiyo imetokana na kupungua kwa maambukizi ya virusi vya corona duniani, ambapo hivi sasa masharti hayo yamepunguzwa katika nchi nyingine na hata kuruhusu sekta za biashara kuendelea.

Waziri wa Afya nchini Tanzania Ummy Mwalimu, amesema pamoja na kulegezwa kwa masharti hayo bado Serikali inaendelea kuchukua hatua katika kukabiliana na ugonjwa huo.

“Waziri Ummy amesema kutokana na kupungua kwa maambukizi duniani, Serikali imelegeza masharti ya wasafiri wanaoingia nchini kuanzia kesho trh 17/3/2022 ambapo kunaondolewa hitaji la kuwa na cheti cha kipimo (Negative RT-PCR Certificate) kilichokua kikihitajika hapo awali”

Pamoja na hayo Waziri Ummy amesema, jumla ya watu 803 wamepoteza maisha kwa ugonjwa wa corona huku 33,789 wakiambukizwa tangu kuripotiwa kwa kisa cha kwanza nchini humo.

Amesema kuwa Katika kipindi chote Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo, mashirika yasiyo ya kiserikali, Taasisi za Dini na wanataaluma wa afya na wananchi kwa ujumla imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kukabiliana na ugonjwa huu.

Aidha amesema kuwa katika kipindi hicho serikali imeweza kuongeza wigo wa uchunguzi wa kimaabara wa UVIKO-19, ambapo kwa sasa kuna maabara saba ndani ya nchi zenye uwezo wa kupima UVIKO19 ukilinganishab na Maabara moja ya Afya ya Jamii iliyokuwepo wakati wa kulipuka kwa ugonjwa huo mwezi Machi 2020.

“Maabara hizi ni pamoja na Maabara ya Taifa ya Afya ya Jamii, Maabara katika Hospitali za Kanda za Bugando, Mbeya na Maabara katika Hospitali za Rufaa za Mikoa ya Dodoma, Arusha, Kigoma, na Maabara iliyopo katika Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro.

“Aidha, Serikali imesimika mitambo 15 ya hewa tiba ya Oksijeni katika Hospitali mbalimbali nchini ili kuweza kutoa huduma za wagonjwa mahututi wanaohitaji uangalizi maalum.

“Serikali pia imeendelea kuikinga jamii kwa kuwezesha upatikanaji wa chanjo ya UVIKO-19 nchini, ambapo hadi kufikia tarehe 12 Machi 2022, jumla ya watu 2,820,545 wenye umri wa miaka 18 na kuendelea, wamepata chanjo kamili dhidi ya ugonjwa huu.

Idadi hiyo ni sawa na asilimia 9.17 ya watanzania 30,740,928 wenye umri wa miaka 18 na kuendelea ambao wanakidhi vigezo vya kuchanja.

“Idadi hii bado hairidhishi kwa kuwa ili tuweze kufikia kinga ya jamii (Heard immunity) tunapaswa kuchanja angalau asilimia 70 ya watu wenye umrii wa miaka 18 na kuendelea”- Amesema Waziri Ummy.

Amesema kwa Kuzingatia hali hiyo , Mikoa inahitaji kuongeza juhudi katika kuhimiza wananchi kujitokeza kuchanja.

Hata hivyo amesema kuwa hali ya UVIKO-19 katika wimbi la nne nchini kwa sasa imepungua kwa kiasi kikubwa tokea lilipoanza mwanzoni mwa mwezi Desemba 2021, ambapo kwa mwezi Desemba 2021 jumla ya watu 4,285 walithibitika kuwa na maambuzi ya ugonjwa huu.

Amesema Kwa upande wa mwezi Januari 2022 wagonjwa waliothibitika walikuwa 2,737 na kwa kipindi cha mwezi Februari 2022, jumla ya wagonjwa 401 walithibitika kupata maambukizi ya ugonjwa huu.

Amesena kwamba Kupungua kwa maambukizi mapya ya ugonjwa wa COVID-19 kumeripotiwa pia katika baadhi ya nchi Duniani huku kukiambatana na kulegezwa kwa masharti ya kuzuia kusambaa kwa maambukizi.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted