Sindano ya Cabotegravir, tiba mpya ya kuzuia maambukizi ya VVU

Sindano hiyo inachukua wiki nane kabla ya muathirika kupewa dozi nyingine badala ya tembe za kumeza

0

Shirika la Umoja wa Mataifa la kufanikisha upatikanaji wa dawa za tiba kwa gharama nafuu, UNITAID limetangaza utekelezaji wa mchakato mkubwa wa uvumbuzi wa hivi karibuni katika kuzuia virusi vya ukimwi ,VVU ambao ni sindano mpya  ambayo inachukua wiki nane kabla ya muathirika kupewa dozi nyingine badala ya tembe anazopaswa kumeza kila siku.

Kwa mujibu wa taarifa ya UNITAID sindano hiyo mpya ya Cabotegravir itawapa watumiaji njia mbadala ya vidonge vya kumeza vya kila siku na hivyo kutoa chaguo katika kuzuia kusambaa kwa maambukizi mapya ya VVU na kuboresha huduma kwa wale walio katika hatari kubwa ya kuambukizwa virusi hivyo. 

Mbali ya chaguo shirika hilo linasema sindano hiyo itashughulikia pia ​changamoto zinazowakabili kila siku watumiaji wa tembe ambazo zinapunguza ufanisi wa tembe hizo na pia itapunguza hofu kwamba tembe zitatafsiriwa vibaya kwa ajili ya matibabu ya VVU na kusababisha mtumiaji kuteseka kwa unyanyapaa, ubaguzi, au unyanyasaji kutoka kwa wenza  au wapenzi wao. 

UNITAID imeanza utekelezaji wa mkakati wa sindano hiyo nchini Afrika Kusini huku ikitarjia kwenda pia katika nchi zingine. 

Robert Matiru ni mkurugenzi wa programu za UNITAID anasema kuwa ili kuzuia VVU katika vikundi vilivyo katika hatari kubwa, uwekezaji wa Unitaid nchini Afrika Kusini utawezesha baadhi ya upatikanaji wa mapema wa cabotegravir ya muda mrefu, tiba mpya ya kuzuia VVU ambayo inachukua nafasi ya tembe za kila siku kwa kuchomwa sindano moja mara sita kwa mwaka. 

Unitaid inapanga kuzindua majaribio ya pili ya utekelezaji kwa kiwango kikubwa nchini Brazil katika miezi ijayo. Afŕika Kusini mwa Jangwa la Sahaŕa, maambukizo mapya sita kati ya saba ya VVU kwa vijana ni miongoni mwa wasichana na wanawake vijana ambao wana uwezekano  mkubwa wa kuishi na VVU mara mbili zaidi kuliko wanaume wa rika lao. 

Kukiwa na chaguzi zaidi za kinga ya kabla ya kukabiliwa na maambukizi ,Unitaid inatumai watu wengi walio katika hatari ya kuambukizwa VVU watawezeshwa kudhibiti afya zao.

Matiru ameongeza kuwa nchini Brazil programu inatarajiwa kuyafikia makundi mawili ambayo yako katika kiwango cha juu cha maambukizi na yanayoishi na VVU kwa kiasi kikubwa ambayo ni takriban asilimia 30 watu waliobadili jinsia na asilimia 18 ya wanaume wanaofanya ngono na wanaume wenzao. 

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted