Watuhumiwa wawili wa ugaidi na askari wawili wafariki kwenye ajali nchini Tanzania

Ajali hiyo ilihusisha gari namba T.691 DBQ Scania,  likiwa na tela namba T.865 mali ya Kampuni ya Nyanza Bottling, likiwa linatokea Mwanza lililogongana na gari namba PT.3798 Toyota...

0

Watu wanne wamefariki dunia, kati yao wawili wakiwa ni watuhumiwa wa kesi ya kujihusiha na vitendo vya ugaidi, baada ya gari lililokuwa likiwasafirisha watuhumiwa hao kutoka Geita kwenda Mwanza kugongana na lori la mizigo.

Ajali hiyo ilihusisha gari namba T.691 DBQ Scania,  likiwa na tela namba T.865 mali ya Kampuni ya Nyanza Bottling, likiwa linatokea Mwanza lililogongana na gari namba PT.3798 Toyota Landcruiser mali ya Jeshi la Polisi.

Akizungumuza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, ACP Henry Mwaibambe, amesema ajali hiyo ilitokea jana Jumatano Aprili 27, 2022 majira ya saa 10 alasiri, eneo la Kijiji cha Ibanda, kata ya Kanyala wilayani Geita, barabara ya Geita-Sengerema.

Amewataja waliofariki kuwa ni watuhumiwa wa ugaidi, Twaha Said na Tesha Murushidi, pamoja na polisi wawili wa Mkoa wa Mwanza, ambao ni G.4467 D/CPL Mussa na G.5702 Faraji.

“Watuhumiwa hawa walikuwa wanakabiliwa na kesi namba PI 3/2022 kwa makosa ya kujihusisha na vitendo vya kigaidi na mauaji. Walikuwa wakihifadhiwa  gereza la Butimba Mwanza, kwani gereza la Geita halina uwezo wa kuhifadhi watuhumiwa wa makosa hayo.”

Aliwataja majeruhi wa ajali hiyo ni PF 23158 A/INSP, Baraka Apila na F.8361 D/SGT Berison Sanga, ambao ni askari wa Mkoa wa Mwanza na Maronja Katemi (52), dereva wa lori la Nyanza na Paulo Charles (32) mfanyakazi wa Nyanza.

“Chanzo cha ajali ni gari namba PT.3798 Toyota Land Cruiser, ambayo ilikatika Sterling Rod na kuhama kutoka upande wake na kwenda upande mwingine na kusababisha kugongana na lori la kampuni ya Nyanza Bottling.

“Majeruhi wanaendelea na matibabu katika hospitali ya Mkoa wa Geita na miili ya marehemu ilipelekwa kuhifadhiwa katika hospitali ya Rufaa ya Bugando, Mwanza,” amesema Kamanda Mwaibambe.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted