Ukame katika Pembe ya Afrika huenda ukawasababishia njaa watu milioni 20

Umoja wa Mataifa unasema eneo la Pembe ya Afrika unakabiliwa na ukame mbaya zaidi katika miaka 40.

0
Mizoga ya ng’ombe  ikiwa imetapakaa mjini Dhobley nchini Somalia mnamo Agosti 11, 2011 (Photo by PHIL MOORE / AFP)

Kutoka kusini mwa Ethiopia hadi kaskazini mwa Kenya na Somalia, maeneo mengi katika Pembe ya Afrika yanakabiliwa na ukame ambao unahatarisha maisha ya watu milioni 20.

Mkutano wa wafadhili wiki jana ulikusanya karibu dola bilioni 1.4 kwa kanda hiyo, ambayo Umoja wa Mataifa unasema unakabiliwa na ukame mbaya zaidi katika miaka 40.

Katika maeneo yanayokumbwa na ukame, watu hupata riziki hasa kutokana na ufugaji na kilimo cha kujikimu.

Wanakabiliwa na kiangazi kikali baada ya kukosa mvua kwa msimu wa nne mfululizo tangu mwisho wa 2020 — hali iliyochangiwa na uvamizi wa nzige ambao uliangamiza mazao kati ya 2019 na 2021.

“Idadi ya watu wenye njaa kutokana na ukame inaweza kuongezeka kutoka wastani wa milioni 14 hadi sasa milioni katika mwaka wa 2022,” Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) lilisema mwezi jana.

Wasomali milioni sita — asilimia 40 ya watu — wanakabiliwa na viwango vya juu vya uhaba wa chakula na kuna “hatari halisi ya njaa katika miezi ijayo” ikiwa hali ya sasa itatawala, shirika la Umoja wa Mataifa la kukabiliana na misaada ya kibinadamu OCHA lilisema wiki iliyopita.

Watu wengine milioni 6.5 nchini Ethiopia “wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula, ilisema, pamoja na milioni 3.5 nchini Kenya.

Katika eneo lote, watu milioni moja wamehama makazi yao kutokana na ukosefu wa maji na malisho, na angalau mifugo milioni tatu wameangamia, OCHA ilisema.

“Lazima tuchukue hatua sasa… ikiwa tunataka kuzuia janga la kibinadamu,” mwakilishi wa Shirika la Chakula na Kilimo katika Umoja wa Afrika, Chimimba David Phiri, alisema katika mkutano wa Umoja wa Mataifa mjini Geneva mwezi Aprili.

Wataalamu wanasema hali ya sasa inatokea kwa kuongezeka kwa mabadiliko ya hali ya hewa.

Hali mbaya katika Pembe ya Afrika imechochewa na vita vya Ukraine, ambavyo vimechangia kupanda kwa gharama za chakula na mafuta, kuvuruga ugavi wa kimataifa na kuelekeza pesa za misaada kutoka eneo hilo.

Mkurugenzi mtendaji wa UNICEF Catherine Russell alisema watoto milioni 10 nchini Djibouti, Ethiopia, Kenya na Somalia wanahitaji msaada wa haraka wa kuokoa maisha kwa sababu ya uhaba huo.

“Kwa ujumla watoto milioni 1.7 katika kanda nzima wana utapiamlo,” alisema katika taarifa yake baada ya ziara ya siku nne nchini Ethiopia wiki iliyopita.

Russell alisema ukosefu wa maji safi unaongeza hatari ya magonjwa miongoni mwa watoto, wakati mamia kwa maelfu wameacha shule, wengi wakilazimika kusafiri umbali mrefu kutafuta chakula na maji.

Afrika Mashariki ilivumilia ukame mbaya mwaka wa 2017 lakini hatua za awali za kibinadamu ziliepusha njaa nchini Somalia.

Lakini mwaka 2011, watu 260,000 — nusu yao wakiwa watoto chini ya umri wa miaka sita — walikufa kwa njaa katika nchi hiyo, kutokana na kwamba jumuiya ya kimataifa haikuchukua hatua za haraka, kulingana na Umoja wa Mataifa.

Kando na matokeo ya moja kwa moja na yanayoweza kusababisha vifo kwa watu walioathirika, uhaba wa maji na ardhi ya malisho ni chanzo cha migogoro baina ya jamii, hasa miongoni mwa wafugaji.

Ukame pia unatishia maisha ya wanyama.

Mifugo kama vile ng’ombe — chanzo muhimu cha kujikimu katika eneo hilo — wanakufa kwa wingi.

Wanyamapori pia wako hatarini.

Nchini Kenya, kumekuwa na visa vingi vya wanyama pori kama vile twiga au swala kuangamia kwa kukosa maji na chakula, mizoga yao ikioza kwenye mbuga.

Wakati wa ukame, wanyama pori huacha maeneo yao na kwenda karibu na makazi ya binadamu.

Katikati mwa Kenya, paka mwitu wameshambulia mifugo, huku ndovu na nyati wakienda malishoni katika mashamba, jambo ambalo limewakasirisha wakazi wa eneo hilo.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted