Mwendesha mashtaka wa Chad ataka viongozi wa upinzani wafungwe kifungo cha miaka 2 jela

Maandamano yaliyoidhinishwa mnamo dhidi ya uwepo wa jeshi la Ufaransa nchini Chad yaligeuka kuwa ya vurugu. Vituo vya mafuta vya kampuni ya Ufaransa ya Total vilishambuliwa

0

Mwendesha mashtaka wa umma wa Chad siku ya Jumatatu alisema anapendekeza viongozi sita wa upinzani wanaoshtakiwa kwa kuvuruga utulivu wa umma baada ya maandamano ya kupinga Ufaransa mwezi uliopita kuhukumiwa vifungo vya miaka miwili jela.

 “Tunaomba vifungo vya miaka miwili jela na faini ya faranga 100,000 za CFA” (takriban $160, euro 150) dhidi ya kila mmoja wa washtakiwa, mwendesha mashtaka Moussa Wade Djibrine aliiambia AFP kesi yao ilipokuwa ikiendelea.

Kesi hiyo inakuja huku kukiwa na hali ya mvutano wa kisiasa nchini Chad, ambako jeshi lilikuja madarakani kufuatia kifo cha kiongozi mkongwe wa nchi hiyo miezi 14 iliyopita.

Maandamano yaliyoidhinishwa mnamo Mei 14 dhidi ya uwepo wa jeshi la Ufaransa nchini Chad yaligeuka kuwa ya vurugu.

Vituo saba vya mafuta vya kampuni ya mafuta ya Ufaransa ya Total vilishambuliwa na polisi 12 walijeruhiwa.

Baada ya hayo, mamlaka ilitekeleza msururu wa kuwakamata waandalizi wa maandamano hayo, ambao walikana kuhusika na ghasia hizo.

Walioshtakiwa ni pamoja na Max Loalngar, mratibu wa Wakit Tamma, ambao ni muungano mkuu wa upinzani nchini humo, na Gounoung Vaima Gan-Fare, katibu wa shirikisho la vyama vya wafanyakazi nchini Chad.

Sita hao wameshtakiwa kwa kuvuruga utulivu wa umma na uharibifu wa mali.

Uamuzi wa kesi hiyo unatarajiwa kutangazwa Jumatatu katika mahakama ya Moussoro, karibu kilomita 300 kutoka mji mkuu N’Djamena.

Vyama vya wafanyakazi, vyama vya siasa vya upinzani na mashirika yasiyo ya kiserikali ya kimataifa yametoa wito kwa sita hao kuachiliwa mara moja na bila masharti.

Chad imekuwa chini ya utawala wa kijeshi tangu Rais Idriss Deby Itno kuuawa Aprili 2021 wakati wa operesheni za kuwaangamiza waasi kaskazini mwa nchi hiyo.

Alirithiwa na mwanawe Mahamat Idriss Deby Itno ambaye ni jenerali.

Alichukua usukani wa kundi la wanachama 15 wa maafisa wakuu na akateuliwa kuwa rais wa mpito.

Junta ilisitisha katiba lakini ikaapa kufanya ‘uchaguzi huru na wa kidemokrasia’ ndani ya miezi 18 baada ya kuandaa kongamano lililopendekezwa la kitaifa kuhusu matatizo ya nchi.

Uongozi wa nchi na jeshi umekubaliwa na nchi za Magharibi, zikiongozwa na mkoloni wa zamani Ufaransa, ambayo inaiona Chad kama mshirika wa karibu katika mapambano yake dhidi ya wanajihadi katika eneo hilo.

Mapinduzi mengine ya hivi majuzi barani Afrika — nchini Guinea, Mali na Burkina Faso — yamekabiliwa na shutuma au vikwazo vya kikanda.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted