Papa aahirisha ziara ya Afrika kutokana na tatizo la goti

Papa Francis ataahirisha safari yake katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Sudan Kusini kutokana na tatizo la goti, Vatican ilisema

0
Katika picha hii iliyochukuliwa tarehe 08 Juni, 2022 Papa Francis anasaidiwa kuinuka kutoka kwenye kiti chake mwishoni mwa hadhira kuu ya kila wiki mnamo Juni 8, 2022 kwenye Uwanja wa St. Peter’s huko Vatican. (Photo by Alberto PIZZOLI / AFP)

Papa Francis ataahirisha safari yake katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Sudan Kusini kutokana na tatizo linaloendelea la goti, Vatican ilisema Ijumaa.

“Kwa agizo la madaktari wake, na ili kutohatarisha matokeo ya matibabu anayopata kwa goti lake, Baba Mtakatifu amelazimika kuahirisha, kwa masikitiko, Safari yake katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Sudan Kusini,” msemaji wa Vatican Matteo Bruni alisema katika taarifa.

Safari hiyo, iliyopangwa kufanyika Julai 2 hadi 7, itaratibiwa upya ingawa hakuna tarehe mpya iliyowekwa.

Papa Francis, 85, amekuwa akisumbuliwa na maumivu katika goti lake la kulia katika wiki za hivi karibuni na mwezi uliopita alitumia kiti cha magurudumu kwa mara ya kwanza kwenye hafla ya umma.

Ameghairi shughuli nyingi — na kuahirisha safari iliyopangwa ya kwenda Lebanon mwezi Juni — na wakati mwingine ameonekana akijitahidi kutembea.

Vatican haijasema rasmi tatizo ni nini, ingawa vyanzo vimeiambia AFP kwamba ana ugonjwa wa yabisi sugu.

Vatican ambayo ilitangaza safari hiyo barani Afrika mwezi Machi, ilikuwa tayari imechapisha ratiba yake.

Papa huyo alikuwa atembelee mji mkuu wa DRC wa Kinshasa, pamoja na Goma, mji mkuu katika jimbo lenye machafuko la mashariki la Kivu Kaskazini.

Alikuwa kuwa pia aelekee Sudan Kusini, kutembelea mji mkuu Juba.

Sudan Kusini, taifa jipya zaidi duniani, limekumbwa na ukosefu wa utulivu wa kudumu tangu lipate uhuru mwaka 2011, ikiwa ni pamoja na vita vya kikatili vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa miaka mitano.

Wakati huo huo DRC, ambayo Papa John Paul II alitembelea mnamo Agosti 1985, inajitahidi kukabiliana na makumi ya makundi yenye silaha mashariki mwa taifa hilo.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted